DAR ES SALAAM: WAJUMBE saba wa Kamati ya Mawasiliano, Ardhi na Nishati ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar wametembelea makao makuu ya Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA) jijini Dar es Salaam kwa lengo la kujifunza na kupata uzoefu wa namna inavyotekeleza majukumu yake.
Mbali na hilo, wajumbe hao walifanya ziara hiyo juzi (Jumatatu) kujifunza mipango ya utatuzi wa changamoto za sekta ya mawasiliano.

Ziara hiyo iliongozwa na Mwenyekiti wa Kamati, Yahya Rashid Abdulla, ikiwahusisha wajumbe saba kutoka Baraza la Wawakilishi Zanzibar.
Akitoa hotuba yake kwa wajumbe hao, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dk Jabiri Bakari alisema kuwa Mamlaka hiyo imefanikiwa kupunguza gharama za kupiga simu kwenda mitandao mingine, kuongezeka kwa upatikanaji wa huduma za simu na intaneti na kuimarisha usalama wa mawasiliano.
Hata hivyo, wajumbe hao waliipongeza TCRA kwa kusimamia sekta ya mawasiliano nchini na kuahidi kuendelea kuiunga mkono TCRA katika juhudi zake za kuboresha sekta ya mawasiliano.
Naye Mwenyekiti wa Kamati, Abdallah aliwashauri wataalam wa TCRA kuwa tayari na mabadiliko ya teknolojia mpya za sekta ya mawasiliano nchini ili kuhakikisha taifa linakuwa mbele na halibaki nyuma na mageuzi yanayotokea kwa kasi duniani.