Wakabidhi pikipiki kuimarisha usalama Arusha

ARUSHA; KAMPUNI ya Multicable Limited inayojishughulisha na uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za umeme pamoja na masuala ya utalii, imekabidhi pikipiki 10 kwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda kwa lengo la kuimarisha ulinzi na usalama mkoani Arusha ili kukuza utalii.

Pikipiki hizo zimekabidhiwa leo jijini Arusha na Hussein Ali Bhai na Murtaza Ali Bhai, ambao ni wakurugenzi wa kampuni hiyo, huku wakimpongeza Makonda kwa kuendelea kuimarisha ulinzi na usalama mkoani Arusha.

Advertisement

“Sisi Multcable Limited tumekuja kuunga juhudi za Mkuu wa Mkoa wa Arusha katika kampeni yake ya kuufanya mkoa kuwa sehemu salama.Tumeona utendaji wake katika kulisaidia Jeshi la Polisi kufanya shughuli zake na tunaahidi kuendelea kushirikiana na Ofisi yake,” amesema Ali Bhai.

Kwa upande wake Makonda amesema dhamira yake ni kuhakikisha jeshi hilo linafanya kazi kwa ufanisi kwa kuwa na vifaa vya kisasa, vitakavyowawezesha kubaini na kuzuia uhalifu na kuifanya Arusha kuwa kivutio cha wageni na watalii.