MENEJA wa Wakala ya Barabara (TANROADS) mkoani Mwanza, Mhandisi Paschal Ambrose amesema ujenzi wa daraja la Magufuli (Kigongo Busisi) limefikia asilimia 78.
Daraja hilo lenye urefu wa kilomita 3.2 limejengwa na idadi kubwa ya wakandarasi wazawa kati ya 750 hadi 1000 ambapo wakandarasi kutoka nje ya nchi ni 57 tu.
Mhandisi Ambrose amesema hayo Novemba 7, 2023 alipozungumza na waandishi wa habari kutoka mikoa ya Shinyanga, Mara, Geita na Mwanza katika ofisi za Tanroads mkoani humo.
“Mradi wa ujenzi wa daraja hilo ulianza mwaka 2020, mwezi February na kipindi cha miaka miwili na nusu ya uongozi wa Rais Samia Suluhu alikuta ujenzi umefikia asilimia 25 na ameweza kutoa fedha za uendelezaji wa mradi huo wa kimkakati na Sasa umefikia asilimia 78.”alisema Mhandisi Ambrose.
Msimamizi wa ujenzi wa daraja hilo kutoka Tanroads Mhandisi William Sanga alisema likikamilika litakuwa ni daraja kubwa linaloongoza kwa Afrika Mashariki likiwa na urefu wa kilomita tatu pamoja na barabara unganishi kilomita 1.
66 huku kukiwa na njia nne za kupita magari kwenda na kurudi.
Mhandisi Sanga alisema kwa sasa barabara hiyo inaunganishwa kwa kutumia vivuko vikubwa vitatu vya Mv Mwanza,Misungwi na Sengerema na wananchi na magari walikuwa wak itumia masaa mawili hadi manne kuvuka lakini ujenzi ukikamilika watatumia dakika 15 kutembea kwa miguu na dakika tatu kwa gari.
Mhandisi mshauri wa ujenzi huo Abdulkarimu Majuto alisema changamoto ya kuchelewa kwa fedha haipo kwani Serikali imehakikisha inawalipa kwa wakati hilo wanaipongeza.
Katika ziara hiyo mwenyekiti wa Shinyanga press club Greyson Kakuru alisema waandishi kupatiwa fursa ya kutembelea mradi huo ni moja ya njia ya kujifunza na kutoa elimu kwa wananchi kwani ipo miradi mingi ya kimkakati inapaswa waandishi waifahamu .
“Waandishi wa habari ndiyo daraja la kupita kwa jamii kujua nini kinaendelea katika nchi hivyo ninaipongeza Tanroads kuliona suala la ujifunzaji kwa waandishi wa habari ni muhimu na kuhakikisha kuwa mabalozi kuitangaza”alisema Kakuru.