Wanafunzi Handeni, Mkinga kupewa chakula bure shuleni 

WANAFUNZI 28,110 waliopo Wilaya za Handeni na Mkinga, wanatarajia kunufaika na mpango wa utoaji wa chakula  cha mchana shuleni.

Mpango huo ambao unatekelezwa na Shirika la World Vision na Save The Children International unakwenda kutoa huduma ya chakula katika shule za msingi 54.

Akipokea msaada huo, wakati wa uzinduzi wa ugawaji wa chakula uliofanyika wilayani Mkinga,  Mkuu wa Tanga,  Omar Mgumba amesema takwimu za hali ya usalama wa chakula zilizotolewa na Wizara ya Kilimo zimeonesha kuwa Mkoa wa Tanga upo katika hatari ya kupata upungufu wa chakula.

“Wilaya za Mkinga na Handeni ndio zimeonesha kuathirika zaidi na ukame,  hivyo uwepo wa mpango huo unakwenda kutoa uhakika wa wanafunzi kuweza kuhudhuria masomo yao, huku wakiwa na uhakika wa kupata chakula, ” amesema Mgumba.

Amesema kuwa utoaji wa chakula cha mchana utasaidia kuinua ufaulu wa watoto na kuongeza mahudhurio yao, hivyo aliwataka viongozi wa halmashauri hizo kuweka mpango madhubuti wa kusimamia utoaji wa chakula katika shule zote zilizopo kwenye wilaya hizo.

Mkurungenzi Mkuu wa World Vision, Gilbert Kamanga amesema mpango huo wa kugawa chakula unatarajia kuwafikia watoto 28,110 waliopo  shule 54 kwa kipindi cha miezi mitatu kuanzia Septemba hadi Novemba mwaka huu.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button