KIGOMA: Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Thobias Andengenye amewataka wananchi wa mkoa huo kutoa ushirikiano kwa wajumbe (wadadisi) kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) wanaopita kwenye maeneo yao kufanya utafiti wa shughuli za kiuchumi na kijamii.
Andengenye amesema hayo akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utafiti huo unaofanyika mkoani humo ambao Kigoma ni sehemu ya mikoa 26 inayofanya utafiti huo nchini.
Mkuu huyo wa mkoa amesema kuwa utafiti huo utasaidia kupata fremu ambayo itatumika katika tafiti mbalimbali nchini na kwamba kwa serikali kupitia NBS inataka kupata takwimu za wakati huu ambazo zitasaidia serikali na wadau wengine kupanga, kutekeleza na kufuatilia ufanisi wa mipango na programu mbalimbali.
Meneja kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Mkoa wa Kigoma, Suma Robert amesema kuwa utafiti huo utahusisha pia utafiti kuhusu masuala ya kilimo ambacho kinachangia kutoa asilimia 65 ya ajira kwa watanzania na kuchangia asilimia 26 ya pato la Taifa.
Mtakwimu huyo wa Mkoa wa Kigoma amesema kuwa maeneo 25 ya mkoa huo yanataraia kufikiwa huku kila eneo wakikadiria kufikia kaya 18 na kwamba kwa sasa karibu asilimia 60 ya kazi imeshafanyika.