“Wananchi washirikishwe kwenye miradi”

KIGOMA: Wakuu wa idara na watendaji wa Serikali katika  Halmashauri za Mkoa Kigoma wametakiwa kusimamia kikamilifu mpango wa ushirikishwaji wa jamii katika utekelezaji wa miradi ili kuwafaanya wananchi hao kuwa sehemu ya miradi hiyo na kuifanya miradi kuwa endelevu badala ya kufanyiwa hujuma.

Mshauri wa elimu kutika ubalozi wa Uingereza nchini, Dk John Lusingu alisema hayo  kwenye ziara ya kukagua na kufanya tathmini ya hali ya utekelezaji mradi wa Shule Bora mkoani Kigoma ili kujionea hatua mbalimbali za utekelezaji wa mambo yaliyomo kwenye mradi huo.

Dk Lusingu alisema kuwa ushirikishwaji kamili wa wananchi kwenye miradi hiyo hasa inayotekelezwa kwa fedha za wafadhili inajenga taswira ya wananchi kuiona miradi hiyo kuwa ni ya kwao na hivyo kushiriki kuitekeleza, kuilinda na kuitunza hivyo miradi hiyo inakuwa na tija kubwa kwa wananchi kwa muda mrefu.

Advertisement

Akiwa wilayani Buhigwe mshauri huyo alishuhudia mafanikio makubwa katika  baadhi ya shule alizotembelea ikiwa ni pamoja na kuibuliwa kwa shughuli za  uzalishaji mali ikiwemo upandaji wa miti kwa ajili ya miradi ya shule ambapo kwa sasa baadhi ya shule zimeanza kuvuna miti hiyo na fedha zilizopatikana zimeanzisha miradi mingine.