MANYARA: Shirika lisilo la kiserikali la LGCF linalojihusisha na masuala ya kijamii limeandaa kongamano kubwa la Wanawake na Wanaume wanaofanya juhudi katika Mkoa wa Manyara litaloambatana na ugawaji tuzo Machi 2 mwaka huu.
Akizungumza Mkurugenzi wa shirika hilo, Lightness Maina amesema lengo ni kuwapa motisha wanawake na wanaume wanaojitambua kwa uwezo walionao na kuwa na taifa lenye kizazi hai chenye usawa kitachoweza kuzitambua fursa na kutumia ujuzi, maarifa na vipaji katika kujenga jamii yenye maendeleo endelevu.
Amesema lengo lingine ni kuhamasisha wanaume na wanawake kushiriki kwenye shughuli za maendeo na kupinga ukatili wa kijinsia kwa kuwa mkoa huo unatajwa kuongoza kwenye vitendo hivyo pamoja na ukeketaji.
Maina ameeleza kwamba, Kongamano hilo ambalo litaambatana na burudani mbalimbali litafanyika usiku wa Machi 2, 2024 katika hotel ya white rose iliyopo mjini Babati likiongozwa na kauli mbiu isemayo “Kwa Pamoja tunaweza kuifikia dunia”
Katibu wa kongamano hilo Rest George na mjumbe Lucas Mondu wamesema tuzo hizo zenye vipengele 26 ni za kwanza kuwahi kutokea mkoani Manyara hivyo ni vyema kila mmoja akajitokeza kuzishuhudia.