Waomba daraja la kudumu Mto Mngeta

Mto Mngeta

WANANCHI wa vijiji  vya  Lukolongo, Mchombe, Ijia, Mgudeni, Nakaguru na Luvilikila  katika kata ya Mchombe  halmashauri ya Mlimba , wilaya ya Kilombero, mkoani Morogoro wameiomba serikali kuwajengea  daraja la kudumu  katika Mto Mngeta  kutokana na lililokuwepo la mbao kusombwa na maji ya mvua.

Walitoa ombi hilo kijijini hapo  kufuatia  daraja la mbao katika mto huo lililokuwa linaunganisha vijiji hivyo kukatika na kusombwa na maji ya  mvua  yaliyojaa kwenye Mto Mngeta.

Mkazi wa Kijiji cha Mchombe,  Seralina Daudi amesema  daraja hilo  la mbao  lilisombwa  na maji tangu Aprili 11, mwaka huu  na kuleta   adha kubwa kwao kushindwa kuvuka kutoka upande mmoja kwenda mwingine .

Advertisement

Hivyo kutokana na  adha hiyo, waliiomba serikali kuwajengea daraja imara la  chuma litatkalodumu kwa muda mrefu na litakalokuwa ni mkombozi wa  kuviunganisha vijiji vyao .

“ Mfano ukiwa na mgonjwa anayehitaji kufikishwa Hospitali upande wa pili  wa mto , mgonjwa aliyepungukiwa maji mwilili ama damu  inakuwa ni shida  kumvusha yeye  na wasindikizaji  kwa  wakati mmoja, “ amesema Seralina.

Naye mkazi wa Kijiji hicho Ridiwani Kilala,  amemwomba Rais Dk Samia Suluhu Hassan awatatulie changamoto hiyo kwa kujengewa daraja la kudumu litakalokuwa ni chachu kwao  kushiriki kikamilifu shughuli za  maendeleo yao ya  kiuchumi.

Nao baadhi ya wenyeviti wa vijiji hivyo, akiwemo wa kijiji cha  Lukolongo , Aniadi Kateule  kwa nyakati tofauti wamesema  kuwa kukatika kwa daraja hilo kumesababisha shughuli nyingi za kijamii na kiuchumi kukwama kwenye vijiji hivyo.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Mchombe , Batholomeo Swalla amemuomba  Rais Samia  kusaidia uwezeshaji wa kupatikana daraja la chuma litakayokuwa imara .

“  Hapa kuna zaidi ya watu 1,000 wanavuka kila siku kwenye daraja lililokuwepo na baada ya kusombwa na maji kumeathiri shughuli za kijamii na kimaendeleo, “ amesema  Swalla

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *