DURBAN, Afrika Kusini: Watu sita wanashikiliwa na polisi nchini Afrika Kusini wakihusishwa na mauaji ya Rapa Kiernan Jarryd Forbes maarufu “AKA” na meneja wake Tebello “Tibz” Motsoane maarufu “Tibz” waliopigwa risasi na kufariki dunia eneo la barabara ya Florida, Morningside, mjini Durban, February 10, 2023.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa makao makuu ya polisi mjini Durban nchini humo usiku wa kuamkia leo. Waziri wa polisi wa Afrika Kusini Bheki Cele amesema watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani Alhamisi wiki hii.
Akizungumza katika mkutano huo Mkuu wa mkoa, Luteni Jenerali Nhlanhla Mkhwanazi alisema tukio hilo la kusikitisha lilipangwa na washukiwa hao kwa ustadi mkubwa
“Washukiwa hawa sita walikuwa na majukumu tofauti wakati wa operesheni kuna mratibu, ambaye kimsingi ndiye mkuu wa kila kitu, yuko chini ya ulinzi. Tuna wapiga risasi wawili. Tuna watazamaji wawili mmoja wa wao alikuwa ndani ya mgahawa akimfuatilia. Bw Forbes (AKA) na marafiki zake pia tunaye mratibu wa bunduki na magari, kwa sababu gari lililotumika kutoroka eneo la tukio na bunduki zilizotumiwa kupiga risasi, vyote walikodiwa,” Mkhwanazi alisema.
Tukio hilo lililozima ndoto za AKA lilifanyika nje ya mgahawa wa Wish on Florida February 10 mwaka jana na lilinaswa kwenye picha za CCTV na kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii.
Polisi walisema AKA na Motsoane walikuwa wakielekea kwenye gari lao walipovamiwa na watu wawili wenye silaha ambao walivuka barabara na kuwafyatulia risasi kwa karibu. Hata hivyo watuhumiwa hao hawakutajwa majina licha ya kuhusishwa na matukio mengine ya mauaji.