Watakiwa kubadili mtazamo sekta ya kilimo

WANAWAKE na vijana wametakiwa kuacha mawazo kuwa kilimo ni lazima kushika jembe la mkono na kulima, bali waangalie fursa zilizopo katika mnyororo mzima wa thamani katika kilimo.
Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), Dk Geofrey Mkamilo amesema hayo kwenye maonesho ya 47 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF).
Dk Mkamilo alisema makundi hayo maalum yanaweza kujiingiza kwenye usindikaji wa mazao kama korosho na kupata siagi na bidhaa nyingine mbalimbali za korosho badala ya kwenda kulima kwa kutumia jembe la mkono.
“Kijana ama mwanamke anaweza kuingia kwenye eneo la usindikaji katika kuongeza thamani na sio kwenye korosho tu, bali hata kwenye mazao mengine kama zabibu na mpunga,” alisema.
Alisema taasisi hiyo ipo katika maonesho hayo ili kuonyesha wananchi teknolojia na fursa mbalimbali zilizopo, kuwashauri wanaweza kuwekeza wapi, zao gani, na teknolojia ipi itumike katika mnyororo mzima wa thamani katika kilimo.
“TARI tuna teknolojia zilizopo kwenye mazao ya kimkakati na mengineyo kama alizeti, ngano, mkonge, mchikichi, korosho, pamba na mazao mengineyo,” alisema.
Aliongeza kuwa kilimo hivi sasa ndio kila kitu kwani hata bajeti ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka wa fedha 2023/24 ni kubwa inakaribia sh trilioni moja.
“Serikali hii leo tunazungumzia karibu trilioni moja kwa sababu kilimo ni muhimu,” alisema.
TARI inafanya kazi kwa mtandao wa vituo 17 vya utafiti wa kilimo nchini katika ikolojia mbalimbali.