Watakiwa kutumia kalamu kupata viongozi wanawake

Wanahabari wakiwa kazini

WADAU  wa habari wameaswa kutumia kalamu zao kubadilisha mitazamo kwenye vyombo vya  siasa, ili waweze kuongeza nafasi za wanawake viongozi ambao wana sifa za kuongoza katika ngazi zote za jamii.

Wadau wa habari wa masuala ya jinsia na uongozi wamesema hayo katika kongamano la maadhimisho ya miaka 30 ya Uhuru wa  Vyombo vya Habari Duniani yaliyofanyika mjini Unguja

Wamesema ili kubadilisha mitazamo hiyo ni muhimu waandishi wa habari wafahamu matumizi sahihi  ya TEHAMA, ambayo  kwa sasa ni kipaumbele katika maendeleo.

Advertisement

“Tukaanze  kudesign miradi iliyokuwa salama ambayo itawajengea uwezo wanawake waweze kutumia digital salama, ili waweze kufanya uongozi wao, kwa uongozi sisi hatuwezi kutofautiana na watu wengine ila tunawachochea wanawake wawe wajasiri katika kuongoza,wawe na fikra chanya katika kutatua changamoto katika jamii, hivyo vyote wavifanye wakiwa na intaneti,” alisema  mwakilishi wa Shirika la Policy, Navina Mtabazi.

Akichangia  suala hilo la uongozi, Katibu  Tawala Wilaya ya Korogwe  mkoani  Tanga, Rahel Mhando amesema suala la uongozi linahitaji uwe na taarifa na maarifa  sahihi ambayo yataweza kukujenga na kukuongoza katika  shughuli za uongozi

“Kuna mabadiliko mengi ya teknolojia , kuna mabadiliko ya sheria  kuna mabadiliko ya sera, kuna miongozo na taratibu  kadha wa kadha kuligama ma teknolojia  zilizopo kulingana na maisha yanavyoenda duniani tunaadopt vitu vingine  kwa hiyo lazima uwe na maarifa,” alisema  Mhando.

Kwa upande wake mwandishi wa habari na Mtangazaji kutoka  Shirika la Utangazaji Zanzibar ZBC, Kauthar Isaack,  amesema kuna utamaduni uliojengeka  kwa wanawake wengi nchini kuogopa kushindana katika masuala ya kugombea uongozi.

“Kwanza kuna wanawake ambao wao tayari  wanaona  kwamba kuna mila na desturi malezi na makuzi yaliyotukuza tamaduni zetu kweli anaweza kuwa,” alisema Kauthar

Naye mwandishi wa habari na mtanagzaji mkongwe kutoka  kituo cha utangazaji cha Channel Ten, Easther  Zelamula aliwashauri waandishi wa habari wanawake  wasikate tamaa pale wanapokumbana na  vikwazo kazini

“Kwanza ni lazima ujitambue ujithamini self confidence, yaani ujiamini wewe mwenyewe kwani wewe ni nani na kwa nini upo hapo nahata katika utekelezaji wa majukumu yako ni lazima ufanye kwa ufasaha bila kujali maneno ya watu, bila ya kujali pingamizi ya aina yoyote, ili mradi unajielewa na unasimama katika mstari na unajua unachokifanya, basi utakuwa kiongozi mzuri,” alisema Easther.

Katika kongamano  hilo wajumbe wamekubaliana kwamba waandishi wa habari wawe ni wabeba maono kufanikisha  lengo la ongezeko la viongozi wanawake nchini.

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *