ZAIDI ya mashirika 4,000 yasiyo ya kiserikali (NGOs) yamefutiwa usajili Januari 2023 kutokana na kutokidhi matakwa ya kisheria ya kuendesha mashirika hayo pamoja na kutolipia ada mashirika kwa miaka miwili mfululizo.
Wakili wa serikali Ofisi ya Msajili Mashirika yasiyo ya Kiserikali, Faki Shaweji amesema hayo wakati akitoa mafunzo ya kisheria juu ya uendeshaji wa mashirika yasiyo ya kiserikali kwa wakurugenzi wa mashirika hayo na kuwataka kuendelea kufuata sheria za kuendesha mashirika na kujiepusha na mikataba ya wafadhili, ambayo inaweza kuvunja mila na desturi za kitanzania.
Alisema kuwa Msajili wa Mashirika kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali za serikali anaendelea kupitia mashirika zaidi ya 8,000, ambayo hayajafutiwa usajili kuona kama yote yanakidhi vigezo vya uendeshaji wa mashirika, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha mashirika hayo hayajinufaishi yenyewe badala yake wanaisaidia jamii.