SHIRIKA la Umeme nchini (Tanesco), limesema ni wateja 7,000 tu, ambao bado hawajaunganishiwa umeme kati ya wateja karibia 100,000 waliokuwa wamelipa kuunganishiwa huduma hiyo Januari mwaka huu.
Hata hivyo shirika hilo limeahidi hadi kufikia mwishoni mwa mwezi huu, wateja hao wote watakuwa tayari wameunganishiwa huduma hiyo.
Hayo yamesemwa leo na Kaimu Mkurugenzi wa huduma kwa wateja wa shirika hilo, Martine Mwambene wakati wa uzinduzi wa wiki ya huduma kwa wateja iliyofanyika ofisi za shirika hilo mkoani Mwanza.
‘’Mpaka Januari mwaka huu tulikuwa na wateja 90,000 hadi 100,000, waliolipa Sh 27,000 kuunganishiwa umeme na mpaka mwezi Septemba mwaka huu tumebakiza wateja 7000 tu kwa nchi nzima,’’ amesema Mwambene na kuongeza kuwa hadi mwishoni mwa Oktoba wateja hao watakuwa wamepata umeme.
Meneja wa Tanesco Mkoa wa Mwanza, Said Msemo, amesema amesema shirika lao lipo katika mpango wa kujenga kituo kipya cha kupooza umeme katika maeneo ya Usagara mkoani Mwanza.