DAR ES SALAAM: WATOA huduma Nchini wametakiwa kujikita katika matumizi ya teknolojia ya akili bandia ili kurahisisha upatikanaji wa huduma na kutatua changamoto za watumiaji kutokana njia hiyo kuonyesha mafanikio makubwa katika Nchi mbalimbali.
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Jukwaa la Watumiaji Tanzania (TCF) Daud Daud wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es salaam kuhusu maadhimisho ya siku ya haki za mtumiaji duniani ambayo yanafanyika Machi 15 na kitaifa yatafanyika jijini Dar es salaam.
Ameongeza kuwa maadhimisho hayo yatawakutanisha wadau mbalimbali ambapo watajadili masuala mtambuka yanayowahusu watumiaji wa huduma zinazodhibitiwa na zisizodhibitiwa lengo likiwa ni kuhakikisha maslahi ya mtumiaji yanazingatiwa.
Katibu Mtendaji wa Baraza la Watumiaji wa TCRA CCC, Marry Shayo amesema kutokana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia yanayoendelea hivi sasa suala la akili bandia ni muhimu katika kuharakisha huduma pamoja na masuala ya usalama.
Kauli mbiu ya maadhimisho hayo mwaka huu inasema Akili Mnemba inayozingatia Haki na Uwajibikaji wa Mtumiaji ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Albert Chalamila.