MKUU wa Mkoa wa Tanga Omar Mgumba amewasimamisha kazi watumishi wa umma 21 kwa kuhusika katika tukio la moto lililochoma ghala ya kuhifadhia bidhaa za magendo katika Bandari ya Tanga mnamo mwezi Oktoba mwaka huu.
Uamuzi huo aliutoa wakati akipokea ripoti ya uchunguzi kuhusu tukio hilo kutoka kwa Kamati aliyoiunda kuchunguza chanzo cha tukio hilo.
Amesema kuwa watumishi hao wamesimamishwa kazi ili kupisha uchunguzi kutokana na kuitia hasara serikali baada ya tukio hilo huku akiliagiza jeshi la Polisi mkoani hapa kuwakamata wafanyabiasha watatu ambao nao waliohusika kwenye tukio hilo.
Amesema kuwa watumishi hao ni kutoka katika Mamlaka ya Bandari Tanga, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na watumishi kutoka kampuni ya ulinzi ya SUMA JKT wanatuhumiwa kwa makosa ya uzembe ikiwemo kutowajibika katika utekelezaji wa majukumu yao
“Watumishi hao wote wasimame kazi ili kupisha uchunguzi na iwepo ikibainika wamehusika basi hatua kali za kisheria ziweze kuchukuliwa ikiwemo za kinidhamu kwa watumishi watakaohusika kwani hujuma hiyo imeweza kusababisha hasara kubwa kwa serikali.”Amesema Mgumba