MWANZA: JAMII imetakiwa kuachana na mila potofu ya ndoa za utotoni. Wito huo umetolewa leo na mratibu wa mradi wa ‘Hapana marefu yasio na mwisho’ Julia Robert wakati wa uzinduzi wa mafunzo ya kutokomeza ndoa za utotoni.
Mafunzo hayo yameanza leo na yanatarajiwa kumalizika February 16 mwaka huu. mpangoo huo ni wa miaka mitatu na ulianza Julai 2023 na unatarajia kumalizika April 2026. Amesema mradi huo unasimamiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Mashariki ya Ziwa Victoria.
Amesema wanufaika wa mradi huo ni viongozi wa dini mbalimbali pamoja na walimu wa shule za msingi kutoka wilaya 30 za Tanzania bara (Mwanza,Morogoro,Dodoma na Tabora) na Visiwani(Pemba na Unguja).
Amesema katika semina hiyo wanafuaika watafundishwa kuhusu sheria za ndoa, Uislamu na Ukristo na ndoa za utotoni.
‘’Tatizo la ndoa za utotoni bado ni kubwa sana na pia kumekuwa na watoto wengi wamekuwa wanashindwa kuendelea na masomo yao’’ amesema.
Naye Askofu mkuu wa Dayosisi Mashariki ya Ziwa Victoria, Andrew Gule amesema mila nyingi zimekuwa zikiwaumiza sana wanawake na wasichana.
Gule ameiomba Serikali kuangalia upya sheria za ndoa ya utotoni za kuzibadilisha.
Naye Mjumbe wa Kamati ya maridhiano Wilaya ya Mpwapwa Mkoa wa Dodoma, Kitundu Yohana amesema katika wilaya yao, tatizo la ndoa za utotoni bado ni kubwa sana na watoto wengi wamekuwa wanawahi kuolewa kabla ya muda.
Amesema wazazi wengi wanawahi kuozesha watoto wao ili waweze kupata kipato.