Waziri Mavunde awapa neno wadau wa madini

WAZIRI wa Madini, Anthony Mavunde amesema serikali itahakikisha inasimamia kwa ufanisi kampuni zote za uwekezaji kwenye sekta ya madini ziweze kutekeleza kwa vitendo sheria ya uwezeshaji wazawa.

Mavunde amesema hayo mbele ya wadau wa madini mjini Geita baada ya kutembelea kampuni ya mzawa ya BlueCoast Investment Limited inayotoa huduma ya usafiri katika mgodi wa Geita Gold Mining Limited (GGML).

Amesema sheria ya madini ya uwezeshaji wazawa iliyofanyiwa marejeo mwaka 2019 sura ya 213 kifungu cha 102 na 112 inatoa fursa kwa Watanzania wengi zaidi kushirki moja kwa moja kwenye uchumi wa madini.

Advertisement

Amempongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bluecoast, Athanas Inyasi (Mzee Inyasi) kwa kunufaika na mabadiliko ya sheria hiyo ya madini na kuwataka Watanzania wengine kuitumia fursa hiyo kwa ufasaha.

Mavunde amesema uwepo wa sheria ya uwezeshaji wazawa imepunguza malalamiko na migogoro iliyokuwepo kwenye maeneo mengi miaka kadhaa hapo nyuma, kwani Watanzania hawakuweza kunufaika na sekta ya madini.

Amezitaka kampuni za kitanzania kujiandaa kupata fursa kwenye maeneo mbalimbali katika madini kwa kujizatiti kutoa huduma bora na zenye viwango vya kimataifa, ili kutoa ushindani wa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

“Nichukue fursa hii kuwaomba Watanzania wajitokeze kwa wingi pindi nafasi hizi zinapotangazwa na itakuwa kipimo chetu pia cha kuanza kujiandaa kuanza kutoa huduma na kuzalisha bidhaa kwa viwango vya kimataifa,” amesema.

Ameziomba taasisi za kifedha kuunga mkono sheria ya uwezeshaji wazawa kwa kutoa mikopo kwa kampuni binafsi za kitanzania, ili waweze kupata mitaji na kukidhi kiwango na uwezo wa kutoa huduma kwa ubora zaidi.

Mkuu wa Mkoa wa Geita Martin Shigela amesema utekelezaji kwa vitendo sheria ya uwezeshaji wazawa imepanua uwigo wa uwekezaji kwa wazawa na kuiomba serikali kutoa kipaumble kwa kampuni zinazosimamia zaidi sheria hiyo.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Blue Coast Investment Limited, Athanas Inyas ameshukuru serikali kwa sheria ya uwezeshaji wazawa kwani imekuwa chachu ya wao kukua na kupata fursa ya kupata fursa kwenye mgodi mkubwa wa GGML.

2 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *