MKUU wa Wilaya ya Kahama, mkoani Shinyanga, Festo Kiswaga, amewataka maofisa utumishi wa halmashauri za wilaya hiyo, kuhakikisha wanakuwa na utaratibu mzuri kwa walimu, ambao wamekaribia kustaafu na kupanda madaraja, ili waweze kupata stahiki zao mapema.
Kiswaga ameyasema hayo leo alipokuwa mgeni rasmi kwenye mkutano mkuu wa Chama cha Walimu (CWT), kilichowakutanisha wajumbe 2500.
Kiswaga amesema kuwa serikali imeweza kushughulikia matatizo ya mishahara ya walimu, hivyo maofisa utumishi wafuate utaratibu uliopo, wasikwamishe inapofika mwalimu anatakiwa kupanda daraja apande mara moja.
“Nanyi walimu msije kwenye ofisi ya mkuu wa wilaya au mkurugenzi mna shida mkapanga foleni, mnatakiwa kupita moja kwa moja mkatekelezewe shida zenu.
“Nikikuta mwalimu umepanga foleni na wanafunzi wanakusubiri shuleni kufundishwa, nitajua umekuja kupumzika umechoka kufundisha, “amesema Kiswaga.