Sh bilioni 3 kujenga miundombinu ya shule Tanganyika

HALMASHAURI ya Wilaya ya Tanganyika Mkoa wa Katavi kwa mwaka wa fedha 2022/2023 imepokea zaidi ya Sh bilioni 3 kutoka Serikali Kuu na zingine kutoka mradi wa ‘BOOST’ zitakazotumika kujenga na kuboresha miundombinu ya shule za msingi na awali.
Akitoa taarifa ya mapokezi ya fedha hizo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Tanganyika, Shaban Juma amesema fedha hizo zimegawanyika katika sehemu mbili ambapo bilioni moja ni kutoka Serikali kuu na bilioni 2.
28 kutoka mradi wa ‘BOOST’.
Amesema bilioni moja kutoka Serikali Kuu itatumika kujenga shule mpya nne na ujenzi wa madarasa nane katika shule za Kafisha (2), Kambanga (2), Ifinsi (2) na Mnyagala (2)
“Fedha hizi zitatumika katika ujenzi wa Shule mpya nne ambazo ni Shukula, Kasekese, Kawambwa na Lake Tanganyika na kila shule itaghalimu shilingi milioni mia mbili na kila darasa litaghalimu shilingi milioni ishirini na tano”
Aidha, amesema kuipitia fedha za mradi wa BOOST jumla ya kata 11 zitaguswa na mradi huo kati ya Kata 16 za Halmashauri hiyo kwa kujenga vyumba vya madara 32 yatakayo ghalimu milioni 182, shule mpya zitakazojengwa Kata ya Kasekese na Ikola, madarasa ya shule za awali, ujenzi wa matundu ya vyoo 21 na nyumba za walimu.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika, Onesmo Buswelu ametoa wito kwa wataalamu zikiwemo Taasisi za Serikali kama TARURA, TANESCO, RUWASA kuhakikisha wanafanya upembuzi mapema za nini kinatakiwa ili miradi hiyo itakapokamilika na huduma zote ziwe zimefika.
Pia ametoa wito kwa wazabuni kusoma vizuri maelezo na kuzingatia BOQ inavyoelekeza huku akitoa wito kwa wananchi na wafanyabiashara kuchangamkia fursa hiyo kwa kujiinua kiuchumi.
Nae Mwenyekiti wa Halmashauri ya Tanganyika, Hamad Mapengo kwa niaba ya madiwani amemshukuru Rais Dk.
Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya kuboresha sekta ya elimu na tayari yeye pamoja na madiwani wenzake wameanza kuhamasisha kila Kijiji kiwe na benki ya tofali za kutosha.