KIONGOZI wa Chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe amesifu hatua ya serikali kuliomba Bunge kuidhinisha mkataba wa uendeshaji wa Bandari ya Dar es Salaam.
Zitto amesema chama hicho kinafanya uchambuzi Azimio linalopendekezwa na Serikali kwa Bunge na majadiliano ya awali kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Dubai ili kuiruhusu Serikali kuanza majadiliano na Kampuni inayomilikiwa na Serikali ya Dubai ya DP world kuendesha sehemu ya bandari.
“Kwa kuzingatia sera za chama chetu kuhusu uendeshaji wa miundombinu msingi kama bandari, tutatoa kauli rasmi siku ya Jumapili katika mkutano wetu wa hadhara jijini Mwanza.”ameandika Zitto.
Zitto amesema amemsikia Waziri wa Nishati, Januari Makamba akitamka kuwa Mkataba wa LNG Lindi (HGA) utajadiliwa na Baraza la Mawaziri na kisha kuidhinishwa na Bunge, jambo ambalo amesifu kwa kuzingatia masharti ya Ibara ya 63 (3) (e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.
Wakati swala hilo likiendelea kujadiliwa, Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari ( TPA) Juni 7, 2023 ilikanusha taarifa za Serikali kupanga kuipa Kampuni ya DP World ya Falme za Kiarabu ya Dubai mkatata wa uendeshaji wa shughuli za Bandari ya Dar es Salaam kwa miaka 100.
“Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari inapenda kuwajulishwa wateja, wadau wa kitaifa na kimataifa na umma kwa ujumla kwamba taarifa hizo sio sahihi, ni upotoshwaji unaofanywa kwa makusudi na watu wenye nia ovu ya kukwamisha mipango thabiti ya nchi katika kuongeza ufanisi wa sekta ya bandari.