NAIBU Spika wa Bunge, Mussa Azan Zungu amewataka watanzania kuunga mkono miradi inayokuja nchini na kumsaidi Rais Samia Suluhu Hassan kujenga uchumi wa nchi.
Zungu ameyasema hayo leo Juni 30,2023 katika Maonyesho ya Kimataifa ya Biashara ‘Sabasaba’ alipotembelea banda la Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
Amesema, uchumi wa nchi uliathirika kwenye mlipuko wa Covid na sasa umekua kutoka asilimia 4.7 kwa mwaka 2022 hadi asilimia 5 mwaka huu wa 2023.
Amesema, lengo la Rais Samia Suluhu Hassan ni kufikia uchumi wa asilimia tisa ambao utawezesha kusimamia miradi yote mikubwa ya kimkakati na kupeleka huduma mbali mbali kwa wananchi.
“Miradi mikubwa inayokuja nchini tuiunge mkono, tumsaidie Rais, tuielewe, tupambane tulisaidie taifa letu, tuwasadie wananchi wetu katika huduma mbali mbali kama vile afya, elimu na ajira kwa vijana.
Amesema, mkakati wa Rais Samia ni kuimarisha sekta binafsi ambayo ina mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa katika kupunguza tatizo la ajira nchini, kwa vijana wengi kujiajiri na kuajiri kupitia sekta hiyo.
“Kupitia ujenzi wa miradi ya kimkakati inayoendelea nchini ikiwemo Bwawa la Umeme la Julius Nyerere (JNHPP), reli ya kisasa, ujenzi na ukarabati wa meli mbalimbali, bomba la mafuta (EACOP) na mradi wa kuchakata gesi asilia mkoani Lindi;….. “ni imani yetu serikali kuwa uchumi wa Tanzania utaendelea kuimarika na kuwanufaisha watanzania zaidi na kutuwezesha kupeleka huduma za maji, umeme afya na huduma nyingine muhimu za kijamii.
Aidha, amesema, maonyesho ya sabasaba nchi 16 zimeshiriki, hivyo wawekezaji wengi watakuja kutokana na maboresho ya sabasaba.