Makalla asisitiza ushirikiano mapambano dhidi ya rushwa

ARUSHA: MKUU wa Mkoa wa Arusha, Amos Makalla, amesema mapambano dhidi ya rushwa hayawezi kuachiwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) pekee, akiwataka viongozi, watendaji wa serikali, taasisi za umma na wananchi wote mkoani humi kuwajibika katika kulinda fedha na rasilimali za umma katika miradi ya maendeleo.
Makalla amesema bila ushirikiano wa wadau wote, juhudi za serikali katika kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa zinaweza kukabiliwa na changamoto, ikiwamo ucheleweshaji wa miradi, upotevu wa rasilimali na wananchi kukosa huduma kwa wakati.

Makalla ametoa kauli hiyo leo Agosti 10, wakati akifungua warsha ya wadau wa usimamizi na utekelezaji wa programu na miradi ya maendeleo Mkoa wa Arusha na kukutanisha viongozi na watendaji wa Serikali, halmashauri, taasisi za udhibiti, vyombo vya sheria na wadau mbalimbali wa maendeleo warsha ya siku moja iliyoandaliwa na Takukuru Mkoa wa Arusha kwa kushirikiana na ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo.
Amesema mapambano dhidi ya rushwa yanahitaji mfumo shirikishi unaohusisha Serikali, vyombo vya sheria, taasisi za udhibiti, viongozi wa dini na jamii, kwa kuwa kila upande una wajibu wa kulinda misingi ya haki, uadilifu, usalama na utawala bora.

Amesema mahakama, polisi, taasisi za dini na Takukuru ni sehemu muhimu ya mfumo wa usimamizi wa nchi na kwamba endapo kila taasisi itashindwa kutekeleza wajibu wake, misingi ya utawala bora na uwajibikaji inaweza kudhoofika.
Makalla amewataka watendaji wa Serikali kutotumia ufuatiliaji wa Takukuru kama sababu ya kusimamisha au kuchelewesha miradi ya maendeleo, akisema kazi ya taasisi hiyo ni kulinda fedha za wananchi na kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa usahihi na thamani ya fedha inalindana na mradi husika.

“Tusitumie Takukuru kama chaka la kuchelewesha miradi. Takukuru inapofuatilia mradi, lengo ni kuhakikisha mambo yanaenda vizuri na hakuna fedha za wananchi zinazopotea,” amesema.
Makalla pia alisisitiza kuwa fedha zinazotengwa na Serikali kwa ajili ya miradi ya maendeleo zinapaswa kufika katika maeneo yaliyokusudiwa na kutumika kwa kazi zilizoainishwa, akionya dhidi ya vitendo vya kuzichepusha.
Alisema na kuwataka watendaji wa serikali kuepuka kupokea zawadi, huduma au upendeleo kutoka kwa watu wanaowasimamia au kuwafanyia ukaguzi, akisema vitendo hivyo vinaweza kuathiri uwezo wao wa kufanya maamuzi kwa uhuru na haki.
Kabla ya kumkaribisha Makalla katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha, Dkt. Toba Nguvilla, alisema viongozi Mkoa Arusha wana wajibu wa kuimarisha utawala bora, mapambano dhidi ya rushwa na usimamizi madhubuti wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora.
Awali akitoa taarifa ya Takukuru Mkoani Arusha,Kamanda wa taasisi hiyo Zawadi Ngailo alisema katika mwaka wa fedha 2023/24,2024/25 na 2025/26 Ofisi yake imefuatilia matumizi ya rasilimali za umma katika program na miradi ya maendeleo 164 yenye thamani ya shilingi Bilioni 469.
Ngailo alisema kuwa Miradi 109 ilikutwa na dosari ambazo zilitolewa mapendekezo 452 ya kuiboresha miradi hiyo na mapendekezo hayo yalitolewa kwa wadau kwa njia ya vikao vya warsha na barua kutokana na mapungufu na changamoto katika miradi inayofuatiliwa ndio imekuwa chachu ya uandaaji wa warsha hiyo.



