Dk Kijaji akagua miradi ya Sh bilioni 110.4 Kagera

KAGERA: Waziri wa Maliasili na Utalii na Mlezi wa Mkoa wa Kagera, Dk Ashatu Kijaji, amehitimisha ziara ya siku tano mkoani humo, ambapo ametembelea na kukagua miradi 17 ya maendeleo yenye thamani ya Sh bilioni 110.4 katika halmashauri zote nane za mkoa huo.
Katika ziara hiyo, Kijaji ametembelea, kukagua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali ya maendeleo, pamoja na kufanya mikutano ya hadhara na wananchi katika maeneo aliyoyatembelea.

Akizungumza na waandishi wa habari mkoani Kagera mara baada ya kuhitimisha ziara hiyo, Kijaji amesema watumishi wa Serikali na viongozi waliokabidhiwa dhamana ya kusimamia miradi ya maendeleo wanapaswa kuhakikisha wakandarasi wanakamilisha miradi kwa wakati ili iweze kuanza kutoa huduma na kuleta tija kwa wananchi.
Aidha, ameuagiza uongozi wa Mkoa wa Kagera kuhakikisha miradi yote iliyokamilika inalindwa na kutunzwa ili iweze kudumu kwa muda mrefu na kuonesha thamani halisi ya fedha zilizotolewa na Serikali.

“Mhe. Rais alipowateua viongozi aliona kwamba hawezi kufika kila eneo, hivyo kila Waziri amepewa jukumu la kuwa Mlezi wa Mkoa ili kuangalia miradi kwa jicho la tatu. Mimi ni Mlezi wa Mkoa wa Kagera, ndiyo maana nimefika kuangalia miradi inayotekelezwa,” amesema Kijaji.
Amesema jukumu kubwa la ziara hiyo lilikuwa kuhakikisha miradi inayotekelezwa inazingatia mikataba iliyosainiwa, viwango vinavyotakiwa na inakamilishwa kwa wakati ili kuleta manufaa na tabasamu kwa wananchi.

“Jambo kubwa ni kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa mujibu wa mkataba ili kuacha tabasamu kwa wananchi wote na Watanzania wote. Mimi nitaendelea kuulea Mkoa wa Kagera na kuwa jicho la Mama Samia kwa kila mradi unaotekelezwa,” amesema.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Kanali Yahaya Kidogo, amesema Serikali kwa mwaka wa fedha 2025/2026 imetenga zaidi ya Sh bilioni 400 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani humo.

Amesema fedha hizo ni sehemu ya juhudi za Serikali katika kuendelea kuboresha huduma za kijamii na kiuchumi pamoja na kuongeza kasi ya maendeleo katika Mkoa wa Kagera.



