Kiruswa Jimbo Cup kuongezwa michezo mingine

ARUSHA: NAIBU Waziri wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Longido mkoani Arusha, Dk Steven Kiruswa, amesema mwakani mashindano ya Kiruswa Jimbo Cup yatakuja kwa sura mpya kwa kuongeza michezo mingine, ikiwemo mpira wa pete, mpira wa wavu na mpira wa kikapu, kwa lengo la kuibua vipaji vya vijana.

Kiruswa alisema hayo baada ya kuzindua rasmi msimu wa sita wa Kiruswa Jimbo Cup, mashindano yanayowakutanisha vijana kutoka tarafa zote nne za Wilaya ya Longido na kupata bingwa wa soka wa kombe hilo.

Alisema mwaka huu timu 51 zimethibitisha kushiriki mashindano hayo, huku akiwataka vijana wa kike na kiume wenye vipaji vya mpira wa pete, mpira wa wavu na mpira wa kikapu kujiandaa kushiriki mwakani ili wapate fursa ya kujiendeleza kitaifa na kimataifa.

Alisema Longido ina akademi nzuri ya michezo iliyoanzishwa na mpenda michezo na yenye miundombinu yote ya michezo, hivyo ataweka mkono wake kwa kuanzisha mashindano ya michezo hiyo ambayo yatafanyika kila mwaka, kama ilivyo kwa mashindano ya riadha ya Kiruswa Fun Run na soka yanayojulikana kama Kiruswa Jimbo Cup.

Naibu Waziri huyo alisema mashindano ya Kiruswa Jimbo Cup yamefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kipindi cha miaka sita sambamba na riadha, ambapo vijana wamechukuliwa kwenda kucheza katika ligi za madaraja ya juu na wanariadha kuitwa kushiriki mashindano ya kitaifa na kimataifa.

“Sasa nakuja na michezo mingine nayo nataka iwatoe vijana wa kiume na kike Longido kwenda duniani kushindana na kupata fursa za kimaisha kupitia michezo na kujikita katika michezo zaidi na kuacha mara moja kujikita katika ujambazi, dawa za kulevya na ulevi,” alisema Kiruswa.

Naye, Mwenyekiti wa Chama cha Soka Wilaya ya Longido (LDFA), Obeid Mollel, amesema Kiruswa Jimbo Cup ni mashindano yanayokua mwaka hadi mwaka na vijana wengi wamefanikiwa kusajiliwa katika timu za ngazi mbalimbali mkoani humo na ligi daraja la pili na la kwanza baada ya kuonyesha vipaji vyao katika mashindano hayo.

Mollel alisema timu zote zinazoshiriki zimepewa seti moja ya jezi na mpira, huku washindi wakipata zawadi ya fedha taslimu na medali. Hata hivyo, alisema mwakani utaratibu utabadilika kwa kuongeza zawadi ya fedha kuwa nono, huku timu zitakazoshika nafasi tatu za juu zikipewa jezi na mpira, badala ya timu zote kama ilivyo sasa, hatua ambayo inalenga kuongeza ushindani katika soka.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Longido, Salumu Kally, amesema Kiruswa Jimbo Cup ni mashindano muhimu katika wilaya hiyo kwa kuwa yanawapa vijana ubize na kuwafanya wajikite katika soka badala ya kujihusisha na uhalifu, dawa za kulevya na ulevi.

Kally amempongeza Mbunge huyo na kumtaka kuendelea kuungwa mkono kwa hali na mali katika juhudi zake za kuendeleza michezo wilayani humo.

Naye, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Papa Nakuta, amesema michezo ni sehemu ya ilani ya chama hicho inayosisitiza kuendeleza michezo, hivyo anachofanya Kiruswa ni utekelezaji wa ilani hiyo katika kukuza michezo Jimbo la Longido.

Alisema vijana wanafurahia mashindano hayo ambayo yamekuwa yakionyesha ushindani mkubwa mwaka hadi mwaka.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button