TAKUKURU Arusha yamnasa raia wa Romania kwa wizi wa fedha

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Arusha imemkamata na kumweka rumande raia wa Romania, Constantin Podoleanu (39), kwa tuhuma za wizi wa mamilioni ya fedha kupitia taarifa za kadi za benki na kujipatia fedha kwa njia haramu.

Mtuhumiwa huyo alikamatwa Agosti 20 mwaka huu majira ya saa 4 usiku katika nyumba yake iliyopo Njiro Block D, Kata ya Engutoto, Halmashauri ya Jiji la Arusha, ambapo maafisa wa TAKUKURU walifanya upekuzi na kubaini vifaa mbalimbali vinavyodaiwa kutumika katika uhalifu.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo, Kamanda wa TAKUKURU Mkoa wa Arusha, Zawadi Ngailo, amesema katika upekuzi huo mtuhumiwa alikutwa na mashine sita za POS, kadi mbalimbali za benki, vifaa na kemikali zinazodaiwa kutumika kutengeneza kadi bandia, pamoja na kompyuta mpakato mbili.

Amesema uchunguzi wa awali umebaini kuwa raia huyo wa Romania alikuwa amefungua karakana ya kufanyia shughuli za uhalifu nyumbani kwake.

Ngailo amesema pia katika upekuzi huo zilikutwa stakabadhi mbalimbali za malipo, zikiwemo zenye thamani ya takribani Sh milioni 171.7 na nyingine za malipo ya dola za Marekani 55,987.20.

Aidha, amesema TAKUKURU ilikuta fedha taslimu za Tanzania kiasi cha Sh milioni mbili, noti za Euro 20 pamoja na fedha za Saudi Arabia kiasi cha Riyal 15.

Kwa mujibu wa Kamanda Ngailo, uchunguzi wa awali umebaini kuwa taarifa za kadi hizo za benki zilizoibwa zilihusisha raia wa mataifa mbalimbali nje ya Tanzania, ambao fedha zao zilikuwa zikitolewa kwenye akaunti zao na baadaye kuonekana zimetumika kulipia huduma mbalimbali nchini Tanzania, licha ya wahusika kutowahi kupata huduma hizo katika kipindi husika.

Amesema TAKUKURU Mkoa wa Arusha inaendelea na uchunguzi ili kubaini ukweli na mazingira yote ya tukio hilo, na kwamba hatua stahiki za kisheria zitachukuliwa baada ya uchunguzi kukamilika.

Aidha, TAKUKURU imewataka wananchi kuendelea kushirikiana na taasisi hiyo katika kufichua vitendo vya uhalifu, ikisisitiza kuwa hakuna mhalifu atakayekuwa salama popote atakapojificha, ndani au nje ya nchi.

TAKUKURU imesema itaendelea kuwafuatilia wahalifu na kuhakikisha wanakamatwa ili wakabiliwe na mkono wa sheria.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button