TISEZA, TLS–AYL kuboresha huduma za kisheria wawekezaji

DAR ES SALAAM; Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) imesaini makubaliano ya ushirikiano wa miaka mitatu na Chama cha Mawakili Vijana ndani ya Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS–AYL), yatakayolenga kuimarisha huduma za kisheria kwa wawekezaji, kuwajengea uwezo mawakili vijana na kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

Makubaliano hayo yanatarajiwa kuwawezesha mawakili vijana kushiriki kikamilifu katika utoaji wa huduma za kisheria zinazohusiana na uwekezaji, huku yakifungua fursa zaidi za ushiriki wao katika shughuli za maendeleo ya uchumi na uwekezaji.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya utiaji saini wa makubaliano hayo jijini Dar es Salaam Julai 29, Mkurugenzi Mtendaji wa TISEZA, Gilead Teri, amesema ushirikiano huo utaunganisha nguvu za taasisi hizo katika kuwajengea uwezo mawakili vijana kupitia mafunzo ya sheria za uwekezaji, ujasiriamali na mbinu za kisasa za utoaji wa huduma za kisheria kwa wawekezaji.

Amesema kupitia ushirikiano huo, mawakili vijana pia watashiriki katika maboresho ya sera, sheria na mifumo inayosimamia uwekezaji nchini, hatua ambayo itasaidia kuongeza ufanisi wa huduma kwa wawekezaji na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha kuvutia uwekezaji wa ndani na nje ya nchi.
Teri amesema lengo la makubaliano hayo ni kuhakikisha mawakili vijana wa Kitanzania hawabaki kuwa waandishi wa mikataba pekee, bali wanajengewa uwezo wa kuwa wataalamu wa sheria za uwekezaji watakaoweza kutoa ushauri wa kitaalamu kwa wawekezaji na kuchangia mageuzi ya uchumi wa taifa.

Aidha, amesema ushirikiano huo utapanua fursa za ajira na maendeleo ya kitaaluma kwa mawakili vijana, sambamba na kupunguza gharama za huduma za kisheria kwa wawekezaji kupitia upatikanaji wa wataalamu wengi wenye ujuzi katika masuala ya uwekezaji.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Umoja wa Mawakili Vijana ndani ya Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS–AYL), Wakili Emmanuel Ukashu, amesema wamechagua kushirikiana na TISEZA kwa kutambua kuwa uwekezaji ni miongoni mwa nguzo muhimu za maendeleo ya uchumi wa Tanzania.
Amesema makubaliano hayo ya miaka mitatu yatawapa mawakili vijana fursa ya kupata mafunzo ya kina kuhusu sheria za uwekezaji, kuongeza uwezo wao wa kitaaluma na kushiriki moja kwa moja katika kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini.

Ukashu ameongeza kuwa ushirikiano huo utaimarisha uhusiano kati ya sekta ya sheria na sekta ya uwekezaji, hatua itakayochangia kujenga mazingira yenye uwazi, uhakika wa kisheria na ushindani, ambayo ni muhimu katika kuvutia wawekezaji na kuchochea ukuaji endelevu wa uchumi wa Tanzania.



