TISEZA yafuatilia maendeleo mradi wa kahawa Mbeya

MBEYA: Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) imetembelea mradi wa uzalishaji wa kahawa wa Utengule Coffee Estate uliopo mkoani Mbeya, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kufuatilia maendeleo ya miradi ya uwekezaji na kuhamasisha uwekezaji wenye tija unaochangia maendeleo ya uchumi wa taifa.
Kwa sasa, mradi huo unazalisha takribani tani 200 za kahawa kwa mwaka na unatarajia kuongeza uzalishaji hadi kufikia tani 250 katika miaka michache ijayo, hatua inayotarajiwa kuongeza mchango wa sekta ya kahawa katika uchumi wa nchi na kuongeza thamani ya mazao ya kilimo.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Meneja wa Kanda ya Juu Kusini wa TISEZA, Fidelis Obanga, alisema mradi wa Utengule Coffee Estate ni mfano wa uwekezaji wenye manufaa kwa wananchi kutokana na mchango wake katika uzalishaji, ajira na uhamishaji wa teknolojia.
“Mbeya ina ardhi yenye rutuba na fursa kubwa za uwekezaji hususan katika kilimo cha kahawa na mazao mengine ya kimkakati.

Mbali na kuongeza uzalishaji wa kahawa, mradi huo umeendelea kuwa chanzo muhimu cha ajira kwa Watanzania kwa kutoa ajira za kudumu zaidi ya 100, huku ukiajiri kati ya watu 200 hadi 500 wakati wa msimu wa mavuno.
Aidha, matumizi ya teknolojia za kisasa katika uzalishaji yamechangia kuwajengea uwezo wafanyakazi wa Kitanzania kupitia mafunzo ya vitendo na uhamishaji wa ujuzi.


