Kairuki apongeza upanuzi huduma za intaneti

DAR ES SALAAM: Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, amesema upanuzi wa huduma za intaneti kupitia mkongo wa Taifa wa fiber optic ni hatua muhimu ya kufungua fursa za elimu, ajira, biashara, ubunifu na huduma bora kwa wananchi

Kairuki amesema hayo Leo wakati wa uzinduzi wa awamu ya pili ya mradi wa Fiber Mlangoni kwa Mteja (FTTH) wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), akieleza kuwa mradi huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kujenga uchumi wa kidijitali na kuhakikisha teknolojia inakuwa chachu ya maendeleo ya wananchi.

Amesema Serikali inataka kuona miundombinu hiyo ikimuwezesha mwanafunzi kujifunza kwa kutumia teknolojia, mfanyabiashara kufikia masoko mapya na taasisi za umma kutoa huduma kwa wananchi kwa haraka, kwa gharama nafuu na kwa ufanisi zaidi.

Ameongeza kuwa huduma za intaneti zenye kasi pia zinaweza kupunguza gharama na muda ambao wananchi hutumia kusafiri kufuata huduma mbalimbali, hususan pale huduma hizo zinapopatikana kupitia mifumo ya kidijitali.

Aidha amesema hadi Juni 2026, idadi ya watumiaji wa intaneti nchini ilifikia milioni 62.7, huku matumizi ya data yakiongezeka hadi kufikia petabyte 1,041 huku matumizi ya fiber majumbani bado yako katika kiwango cha chiniu ikilinganishwa na idadi kubwa ya watumiaji wa intaneti nchini, akitaja kuwa watumiaji wa fiber majumbani walikuwa takribani 178,904.

Kwa upande Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, Moremi Marwa amesema kutokana na ongezeko la mahitaji ya huduma za intaneti na umuhimu wa mawasiliano katika shughuli za kiuchumi na kijamii, TTCL imeanzisha awamu ya pili ya mradi huo ili kuhakikisha huduma za Fiber Mlangoni kwa Mteja zinapatikana katika maeneo mbalimbali nchini.

Ameeleza kuwa katika awamu ya pili, TTCL inalenga kujenga takribani maunganisho 400,000 ya Home Pass, hatua ambayo inatarajiwa kuongeza jumla ya uwezo wa mtandao wa shirika hadi kufikia takribani maunganisho 750,000 ifikapo Juni 2027.

Aidha, amesema mpango wa TTCL ni kufikisha idadi hiyo hadi takribani maunganisho milioni moja ifikapo Juni 2028, ikiwa sehemu ya mpango wa miaka mitatu wa shirika katika kuimarisha huduma za mawasiliano nchini.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button