Afrika ‘yaamshwa’ utoshelevu rasilimali za nishati

ACCRA, GHANA: Mkuu wa Shughuli za Serikali nchini Ghana Dk Julius Debras ametoa wito kwa nchi za Afrika kuangalia kwa namna gani rasilimali zilizopo zinaweza kujitosheleza kama bara hususani katika sekta ya nishati.
Dkt Debras ametoa wito huo katika maadhimisho ya wiki ya mafuta Afrika yanayoendelea jijini Accra, Ghana wakati akitoa hotuba yake kwa niaba ya Rais wa nchi hiyo, John Mahama.
Dk Debras alisisitiza kuwa kuwa endapo bara la Afrika litakuwa na nishati ya uhakika itasaidia kuinua uchumi lakini suala la ajira pia halitakuwa wimbo kwani kutakuwa na maendeleo ya uhakika ya viwanda.
Aliweka bayana kuwa kwa upande wa Mkondo wa Juu wa Petroli wa Ghana, serikali imeweka mikakati mathubuti kuhakikisha kupitia sekta hiyo wanapata wawekezaji wenye uhakika.
Kwa mujibu wa mkuu huyo, ni lazima kama bara la Afrika kuangalia aina ya wawekezaji wanaokuja kuwekeza katika nishati ni lazima wawe na nguvu ya kiuchumi ili kuweza kuleta manufaa ya uhakika na haraka katika sekta hiyo.
Kwa upande wake Kamishna wa Miundombinu na Nishati kutoka Kamisheni ya Umoja wa Afrika, Lerato Mataboge alisema kuwa vijana wa Afrika wapo tayari katika mabadiliko ya nishati yanayoendelea barani Afrika.

Alishauri kuwa kinachotakiwa hivi sasa ni mshikamano wa Afrika kuweka njia madhubuti katika kuhakikisha kuwa katika kuelekea maendeleo hayo kuwe na mabadiliko makubwa katika matumizi ya teknolojia kwa kutoa vipaumbele katika bunifu zote zinazofanywa na vijana wa Afrika.
Alifafanua kuwa Umoja wa Afrika (AU) umeweka utengamano wa viwanda ili kuhakikisha kuwa kunakuwa na ushirikiano wa kikanda katika sekta ya nishati ambao baadaye utaleta tafsiri sahihi ya kuwa na nishati ya uhakika katika bara zima.
Wiki ya Mafuta barani Afrika iliadhimishwa Septemba 2-3 ambapo Tanzania imewakilishwa na wajumbe kutoka Wizara ya Nishati, wajumbe kutoka Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA), na wajumbe kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Petroli Zanzibar (ZPRA).


