DAKTARI bingwa wa magonjwa ya watoto kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, Dk Mwita Ngutunyi amesema mila na desturi za kumwachisha mtoto maziwa ya mama pale anapokuwa mjamzito kwa madai yataleta madhara inawatesa watoto.
Dk Ngutunyi alisema hayo jana katika mada ya hali ya lishe na huduma kwa watoto alipokuwa kwenye mafunzo ya wataalamu wa afya, maofisa lishe na ustawi wa jamii kutoka Kanda ya Ziwa iliyojumuisha mikoa ya Mara, Mwanza, Simiyu, Geita na Shinyanga.
“Mila ya kumwachisha mtoto akiwa na miezi kadhaa wakati mama akiwa mjamzito ni hatari inasumbua, hivyo wazazi wanaweza kutumia mbinu ya uzazi wa mpango kupangilia ili watoto wao waendelee kuwa na afya nzuri na mzazi arudishe afya yake,” alisema.
Dk Ngutunyi alisema wazazi wasipotumia uzazi wa mpango, ukuaji wa mtoto unakuwa sio mzuri na kumrudisha mtoto nyuma.
Ofisa Lishe Mkoa wa Shinyanga, Denis Madeleka alisema asilimia 71 ya watoto chini ya umri wa miaka mitano mkoani Shinyanga wana upungufu wa damu ikiwa baadhi ya wazazi wamekuwa hawanyonyeshi kwa utaratibu unaotakiwa maziwa ya mama ambayo yana virutubisho vingi.