Mtatifikolo atoa mil 1/- kwa kikundi cha wanawake Isimani

IRINGA: MBUNGE wa Jimbo la Isimani, Emmanuela Mtatifikolo, ametoa Sh milioni moja kwa kikundi cha wanawake cha Mwangaza Food Point katika Kijiji cha Mboliboli, Tarafa ya Pawaga, jimboni kwake Isimani, ikiwa ni sehemu ya kuwaunga mkono kuongeza mtaji na kukuza shughuli zao za kiuchumi.

Pamoja na mchango huo, Mtatifikolo aliahidi katika kijiji cha Mbugani kusaidia upatikanaji wa pampu itakayowezesha kusukuma maji kutoka kisimani, huku akitoa Sh 500,000 kama mchango wa ununuzi wa mfumo wa sola utakaotumika kuendesha pampu hiyo.

Misaada hiyo imetolewa wakati wa ziara yake katika vijiji hivyo, ambako pia alisikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi na kuanza kuchukua hatua za kuzitatua.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kikundi cha wanawake, Mtatifikolo aliwapongeza kwa kujikusanya na kuanzisha shughuli za kiuchumi, akisema hatua hiyo inaweza kuongeza kipato cha familia, kuwawezesha kujitegemea na kutengeneza fursa za ajira kwa vijana.

Alisema jitihada za wanawake kushirikiana katika shughuli za uzalishaji ni sehemu muhimu ya kujenga uchumi wa kaya na jamii, hivyo ni muhimu kuendelea kuunga mkono vikundi vinavyoanzisha shughuli zenye tija.

Kwa upande wao, wanakikundi walimshukuru mbunge huyo kwa msaada huo, wakisema fedha walizopewa zitawawezesha kuongeza mtaji na kuimarisha shughuli zao.

Akiwa katika kijiji cha Mbugani, alipokea changamoto ya ukosefu wa maji ya uhakika kwa ajili ya mifugo.

Alisema anaendelea kufuatilia changamoto nyingine zilizowasilishwa na wananchi na kwamba atawashirikisha viongozi mbalimbali wa Serikali, wakiwemo mawaziri wenye dhamana ya kilimo na umwagiliaji, ili kutafuta ufumbuzi wa changamoto hizo.

Katika ziara hiyo, Mtatifikolo alitembelea Kituo cha Afya Mboliboli kwa ajili ya kukagua huduma zinazotolewa na kusikiliza changamoto zinazowakabili wananchi pamoja na wahudumu.

 

Miongoni mwa changamoto alizobaini ni ukosefu wa umeme katika kituo hicho, hali inayokwaza utoaji wa baadhi ya huduma za afya.

Baada ya kubaini changamoto hiyo, mbunge huyo aliwasiliana kwa njia ya simu na Meneja wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Iringa, akiomba hatua zichukuliwe kwa haraka ili kituo hicho kipatiwe umeme.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button