Polisi Arusha wapanda miti Shule ya Msingi Arusha

ARUSHA: Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha limewakumbuka viongozi wakuu wa serikali pamoja na watu maarufu nchini waliosoma katika Shule ya Msingi Arusha, maarufu kama Arusha School, kwa kupanda miti ya matunda na kivuli katika eneo la shule hiyo.

Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya kuwaenzi viongozi na watu mbalimbali waliopata elimu katika shule hiyo kongwe kwa mchango wao mkubwa walioutoa kwa Taifa.

Akizungumza wakati wa zoezi hilo la upandaji miti katika Arusha School, shule iliyoanzishwa mwaka 1934, Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Marijani Mrope, ambaye ni Mkuu wa Polisi Jamii Jiji la Arusha, alisema viongozi waliokumbukwa ni pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Thabit Kombo, mfanyabiashara maarufu nchini Mohamed Dewji, pamoja na watangazaji Salum Kikeke na Millard Ayo.

Mrope alisema yeye pamoja na Polisi Kata wenzake na dawati la jinsia na watoto Wilaya ya Arusha walifika shuleni hapo kwa ajili ya kupanda miti hiyo ikiwa na malengo mawili ya kutunza mazingira na kuenzi viongozi, mashujaa na watu mbalimbali waliopita katika shule hiyo maarufu.

Alisema Arusha School imekuwa kama mti mkuu uliootesha matawi yaliyoleta kivuli na matunda mema kwa Taifa na dunia kwa ujumla, hivyo upandaji wa miche hiyo unaonesha kuthamini mchango wa waliowahi kusoma katika shule hiyo.

Kwa mujibu wa Mrope, viongozi hao walikuwa kama mbegu ndogo zilizopandwa katika shule hiyo, zikakuzwa kwa maarifa na maadili, na baadaye kuwa miti mikubwa yenye kutoa matunda kwa jamii.

Aliongeza kuwa Jeshi la Polisi kupitia kitengo cha Polisi Jamii linaamini kuwa usalama wa raia na mali zao unaendana pia na utunzaji wa mazingira.

 

“Mti mmoja tunaoupanda leo ni alama ya amani, ulinzi na maendeleo endelevu kwa nchi,” alisema Mrope, huku akiwaasa wanafunzi kuwa wao ni mbegu ya kesho na wanapaswa kufuata nyayo za waliowatangulia ili Taifa lijivunie uwepo wao.

Aliwataka Polisi Kata kushirikiana na jamii katika kuhakikisha miti hiyo inalindwa na kutunzwa ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Kwa upande wake, mwanafunzi wa Arusha School, Shaban Ally, aliwashukuru Jeshi la Polisi kwa kufika shuleni hapo na kupanda miti hiyo, akisema hatua hiyo ni njia mojawapo ya kuwaenzi viongozi, watu maarufu na wafanyabiashara waliowahi kusoma katika shule hiyo.

Alisema miti hiyo itatunzwa na kuitaka taasisi nyingine kuiga mfano wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha katika kuhifadhi mazingira na kuenzi historia ya watu waliotoa mchango kwa Taifa.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button