Tanzania kuandika historia mpya uzalishaji umeme

PWANI: WAZIRI wa Nishati, Deogratius Ndejembi, amesema uzinduzi wa mradi wa Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP) ni hatua muhimu katika kuongeza uwezo wa Tanzania kuzalisha umeme na kuifanya nchi kuwa kitovu cha biashara ya nishati katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini.
Akizungumza leo katika uzinduzi wa mradi huo, Ndejembi amesema kituo hicho kina mitambo tisa, ambapo kila mtambo una uwezo wa kuzalisha megawati 235, na kufanya uwezo wa jumla kufikia megawati 2,115.
Amesema ongezeko hilo limeimarisha uwezo wa taifa kukidhi mahitaji ya umeme kwa shughuli za uzalishaji, uwekezaji na ukuaji wa uchumi, huku likiiweka Tanzania katika nafasi muhimu ya kuunganisha masoko ya umeme ya kikanda.
“Tanzania ni mwanachama wa East African Power Pool na Southern Africa Power Pool, ambapo nchi yetu inaunganisha mtandao wa umeme kikanda,” amesema Ndejembi.
Kwa mujibu wa Ndejembi, uwezo wa Tanzania wa kuzalisha umeme umefikia megawati 4,446 dhidi ya mahitaji ya juu ya gridi ya taifa hali ambayo imeiwezesha nchi kuanza kutumia ziada hiyo kwa ajili ya biashara ya umeme.
Amesema Tanzania tayari imeingia makubaliano na Zambia kwa ajili ya kuiuzia umeme, huku ikiwa pia na makubaliano na Kenya ya kuuziana umeme kulingana na mahitaji ya kila nchi.
Ndejembi ameongeza kuwa Serikali inaendelea na mazungumzo na nchi nyingine jirani ili kuuza au kununua umeme pale unapohitajika.



