Mwenge wa uhuru wapongeza ujenzi wa wodi ya wazazi Kakola

SHINYANGA: KIONGOZI wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Wazo Mwang’onda, ameweka Jiwe la Msingi katika jengo la wodi ya wazazi katika Kituo cha Afya Kakola, Kata ya Bulyanhulu, Halmashauri ya Msalala, Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga, lililogharimu zaidi ya Sh milioni 269.

Akisoma taarifa ya ujenzi huo kabla ya kuwekwa kwa jiwe hilo, Mganga Mfawidhi wa kituo hicho, Dk Emanuel Boniface, amesema ujenzi ulianza rasmi Oktoba 2025 na kukamilika Julai 2026.
Amesema Serikali Kuu ilitoa Sh milioni 250 kwa ajili ya ujenzi huo, huku halmashauri ya Msalala ikitoa zaidi ya Sh milioni 19 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya kituo hicho.

Mbunge wa Jimbo la Msalala, Mabula Magangila, amesema kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, Kata ya Kakola ina takribani wakazi 51,000, ambao awali walikuwa wakitegemea zahanati kutokana na kutokuwepo kwa kituo cha afya.

Mwang’onda ameipongeza halmashauri ya Msalala kwa usimamizi mzuri wa ujenzi na wakandarasi, akisema jengo hilo limejengwa kwa kiwango kizuri.

Aidha, ameitaka halmashauri hiyo kuhakikisha miradi mingine inayotekelezwa inasimamiwa kwa umakini ili iweze kukamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya wananchi.



