‘AFCON 2027 ni dhahabu kwa wafanyabiashara’

DAR ES SALAAM: Wafanyabiashara nchini wametakiwa kuanza kujiandaa mapema kutumia fursa zitakazotokana na Tanzania kuwa mwenyeji wa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, kwa kuwa mashindano hayo yanatarajiwa kuongeza shughuli za kiuchumi katika sekta mbalimbali.

Akizungumza Dar es Salaam leo Mkurugenzi wa Masoko wa Photons Energy, Roman Shayo, amesema AFCON siyo tukio la michezo pekee, bali ni fursa kubwa inayoweza kugusa moja kwa moja biashara za sekta mbalimbali, ikiwemo utalii, usafirishaji, hoteli, teknolojia, ujenzi na biashara ndogo ndogo.

Shayo amesema uwekezaji unaofanywa na serikali katika maandalizi ya AFCON unatokana na ukubwa wa fursa zinazoweza kupatikana, hivyo wafanyabiashara wanapaswa kuwa na mtazamo chanya na kuanza kupanga mapema namna watakavyonufaika.

Amesema wamiliki wa hoteli na nyumba za kulala wageni wanaweza kutumia kipindi hiki kuboresha miundombinu na huduma zao, huku wanaojihusisha na usafirishaji wakitakiwa kuongeza uwezo wao ili kukidhi mahitaji yatakayoongezeka wakati wa mashindano hayo.

Kwa wafanyabiashara wadogo, Shayo amesema AFCON inaweza kuongeza mahitaji ya bidhaa na huduma, hivyo ni muhimu kujiandaa kwa kuongeza uzalishaji kulingana na mahitaji ya soko.

“AFCON inapokuja siyo mpira tu. Fursa zake ni nyingi, zinagusa teknolojia, utalii, hoteli, mbuga, mama mboga, barabara, umeme na kila kitu,” amesema Shayo.

Amesema Serikali tayari imefanya sehemu yake kwa kuweka mazingira na kuwekeza katika maandalizi, hivyo jukumu la wafanyabiashara sasa ni kutambua fursa na kujiandaa kuzitumia.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button