Bil 63/- kupeleka umeme GGM Geita

DODOMA: Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba, ameshuhudia utiaji saini wa mkataba wenye thamani ya Sh bilioni 63 kati ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na mkandarasi kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 (kV) kutoka Mpomvu hadi Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM).

Mradi huo pia unahusisha ujenzi wa kituo kipya cha kupokea na kupoza umeme cha 220kV chenye transfoma yenye uwezo wa MVA 90.Hafla ya utiaji saini mkataba huo imefanyika Septemba 3, 2026, jijini Dodoma.

Akizungumza katika hafla hiyo, Makamba amesema mradi huo utatekelezwa kwa ushirikiano wa kampuni za Sihotech Engineering Company na Sieyuan Electric Company Limited, kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa umeme wa uhakika katika maeneo ya migodi na kuchochea shughuli za uzalishaji.

Amesema mradi huo ni sehemu ya Mpango wa Mapato wa TANESCO, unaojumuisha awamu ya kwanza yenye miradi 52 ya usambazaji umeme kwa wateja wakubwa pamoja na miradi mitatu ya usafirishaji umeme inayohusisha maeneo ya migodi.

Makamba amesema hatua ya kuunganisha GGM kwenye Gridi ya Taifa mwaka 2024 ilisaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama za uzalishaji wa umeme pamoja na matumizi ya mafuta.

“Awali GGM ilikuwa ikitumia takribani Sh bilioni 10 hadi 13.4 kwa mwezi kwa ajili ya kuzalisha umeme kwa kutumia mafuta. Baada ya kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa, imeweza kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama hizo,” amesema.

Amesema utekelezaji wa mradi mpya wa msongo wa kilovoti 220 utaongeza uwezo wa kusafirisha na kusambaza umeme kwa GGM, kukidhi ongezeko la mahitaji ya umeme, kuongeza mapato ya TANESCO na kuchochea ajira, uwekezaji na ukuaji wa uchumi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Lazaro Twange, amesema Shirika lilianza kuihudumia GGM mwaka 2024 kwa kuipatia umeme wa MW 16, lakini ongezeko la mitambo na shughuli za uchimbaji limeongeza mahitaji ya umeme na kufanya miundombinu iliyopo kutotosheleza.

Amesema mradi huo utasaidia kukidhi mahitaji yanayoongezeka na kuhakikisha GGM inaendelea kupata umeme wa uhakika kwa ajili ya shughuli zake za uzalishaji.

Naye mwakilishi wa wamiliki wa GGM ameishukuru Serikali kwa hatua hiyo na kuiomba kuhakikisha mradi huo unatekelezwa kwa kasi na kukamilika kwa wakati, ili kuongeza ufanisi wa shughuli za uchimbaji na uzalishaji wa mgodi huo.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button