Kapinga ashuhudia teknolojia bunifu SUA

MOROGORO: WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, ametembelea banda la Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) katika Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki na kujionea teknolojia mbalimbali za kisasa zinazolenga kuimarisha uzalishaji wa mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi.
Akiwa katika banda hilo, Kapinga amepata maelezo kuhusu teknolojia na ubunifu unaofanywa na watafiti wa Chuo Kikuu hicho kwa ajili ya kuwasaidia wakulima, wafugaji na wavuvi kuongeza tija, kuboresha uzalishaji na kuongeza thamani ya bidhaa zao.
Kapinga alijionea teknolojia zinazohusu uzalishaji wa mazao, ufugaji wa kisasa, uvuvi na uchakataji wa mazao, pamoja na bidhaa mbalimbali za kibunifu zinazotokana na tafiti zinazofanywa na chuo hicho.

Waziri Kapinga aliongozwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Mipango, Fedha na Utawala, Profesa Amandus Muhairwa, kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Raphael Chibunda ambapo pia amejionea wanafunzi wa elimu ya amali katika Shule za Sekondari Mafiga Manispaa ya Morogoro uliyopo chini ya usimamizi wa SUA.
Wanafunzi hao wanaonesha uwezo wao wanaoupata kutokana na mafunzo kwa vitendo yanayowapatia fursa ya kujiajiri na kujitegemea wamalizapo masomo
Mwanafunzi wa kidato cha tatu, Jasmin Msemu amesema masomo ya elimu ya amali ni mazuri kwa sababu yampatia fursa kubwa kujiajiri mwenyewe kutokana na kujifunza kwake ufugaji na jinsi ya kutunza shamba la Wanyama.
“Elimu hii inanisadia pia kunutatulia achangamoto kabla sijamaliza shule kutokana na kujikita kwangu kulima bustani za mazao na kuunzwa na kupata fedha za matumizi ya mahitaji mengine yakiwemo ya shule bila kutengemea mzazi,” alisema Amina.

Kwa upande wake Mwalimu wa Amali kwenye somo la Afya ya Wanyama na Uzalishaji wa shule hiyo, Isack Mwamba ameishukuru Serikali kwa kuanzisha mkondo wa amali ,na SUA kwa uwezeshaji walimu kujifunza vitu vingi ikiwemo Kilimo na Mifugo
Shule ya Sekondari Mafiga iliteuliwa na Serikali kupitia Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia kufundisha wanafunzi masomo ya mkondo wa amali katika kilimo eneo la uzalishaji wa mazao, kilimo cha Bustani na mboga , uzalishaji wa wanyama na afya zao.



