Nyaishozi yajipanga mabadiliko chanya sayansi, mazingira

KARAGWE: Shule ya Ushirika wa Wakulima wa Kahawa KDCU Nyaishozi, iliyopo Wilaya ya Karagwe mkoani Kagera, imejikita katika masomo ya sayansi na mazingira kwa lengo la kuwaandaa wanafunzi kutumia maarifa na ubunifu wao katika kutatua changamoto zinazoikabili jamii na kuchochea maendeleo ya sekta ya kilimo.

Shule hiyo, ambayo awali ilianzishwa kwa ajili ya watoto wa jamii ya wakulima wa kahawa wa Kyerwa na Karagwe, kwa sasa imepanua wigo na kupokea wanafunzi kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania.

Katika mahafali yake ya 34 mwaka 2026, jumla ya wanafunzi 255 wanatarajiwa kuhitimu, huku wakiwa na matumaini ya kutumia elimu waliyoipata kujenga maisha yao na kuchangia maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla.

Mwenyekiti wa Chama cha Ushirika wa Wakulima, Fatson Josiah, amesema elimu ya sayansi na teknolojia inaweza kuwa msingi muhimu wa kubadili kilimo kutoka cha mazoea kwenda kilimo cha kisasa, chenye tija na kinachoendana na mabadiliko ya dunia.

Amesema maandalizi mazuri ya watoto kupitia masomo ya sayansi yanaweza kuwajengea uwezo wa kutumia maarifa, vipaji na ubunifu katika kukabiliana na changamoto mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

Josiah amesema licha ya kidato cha nne kuwa hatua ya kawaida katika mfumo wa elimu, ni daraja muhimu linalomuandaa mwanafunzi kwa hatua nyingine za maisha na elimu, hivyo ameiomba jamii ya wakulima kuitumia shule hiyo kama fursa ya kuinua elimu ya watoto wao na kujenga kizazi kitakachokuja kuwa msaada kwa jamii.

Kwa upande wa ushirika, amesema tayari wakulima wamefanya uamuzi wa kuanzisha elimu ya awali katika shule hiyo, huku wakulima wanaozalisha kahawa wakipewa utaratibu wa kugharamia elimu kupitia makato kwenye mauzo ya kahawa badala ya kulipa fedha taslimu.

Amesema utaratibu huo unalenga kuhakikisha watoto wanapata fursa ya kusoma bila kukatishwa masomo kutokana na changamoto za malipo.

Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Audax Gereon, amesema kuanzishwa na kuimarishwa kwa masomo ya sayansi kumekuwa kivutio kikubwa kwa shule hiyo, hali iliyosababisha wanafunzi kutoka mikoa mbalimbali kujiunga nayo.

Gereon amesema elimu inayohusiana na kilimo na mazingira ni muhimu kwa kila mwanafunzi kutokana na nafasi yake katika maisha ya kila siku na maendeleo ya Taifa.

“Kwa mahafali haya ya 34 tunaelezea kielelezo cha mafanikio ya shule kwamba si shule ya wakulima bali ni shule ya Watanzania wote na lengo la shule hii si biashara bali ni huduma kwa watoto na Taifa la kesho,” amesema Gereon.

Diwani wa Kata ya Nyaishozi, Wales Mashanda, amesema amevutiwa na namna wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi wanavyotumia ubunifu wao kutengeneza vifaa mbalimbali kwa kutumia malighafi zinazopatikana katika mazingira yao.

Amesema kupitia mahafali hayo, wanafunzi wameonyesha uwezo wa kubuni na kuwasilisha kazi zao mbele ya jamii, akisisitiza kuwa katika dunia ya sasa, mafanikio ya mwanafunzi hayapaswi kupimwa kwa ufaulu pekee bali pia uwezo wake wa kubuni na kutatua changamoto.

Ametaka watoto wenye vipaji vya ubunifu kupewa nafasi na kuwezeshwa ili waweze kuendeleza mawazo yao na kuibua suluhisho zitakazowanufaisha wao na jamii kwa ujumla.

Katika mahafali hayo, wanafunzi wamewasilisha bunifu mbalimbali, ikiwemo utengenezaji wa magari na roboti, pamoja na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu magonjwa yasiyoambukiza, ikiwemo shinikizo la damu, na umuhimu wa kuzingatia ulaji unaofaa.

Uongozi wa shule umeahidi kuendelea kuzitambua na kuzifuatilia timu za wanafunzi wenye ubunifu, pamoja na kupokea mahitaji na mawazo yao kuhusu vifaa vinavyoweza kuwasaidia kuendeleza vipaji na ndoto zao kupitia masomo ya sayansi.

Kwa hatua hiyo, Nyaishozi Sekondari inalenga kuendelea kuwa kituo cha elimu kinachowaandaa vijana kuwa wabunifu, watatuzi wa changamoto na wazalishaji wa maarifa yatakayosaidia kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button