REA kupeleka umeme vitongoji 16,500 miaka mitatu ijayo

WAKALA wa Nishati Vijijini (REA) umeweka matarajio ya kukamilisha kupeleka umeme katika vitongoji 16,500 kwa kipindi cha miaka mitatu ijayo baada ya kuweka mifumo maalumu ya kuwasimamia wakandarasi waliosaini mikataba namna ya kuwajibika katika utekelezaji wa miradi hiyo ya kimkakati ndani ya muda ulipangwa.
Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy ameema hayo wakati akifungua mkutano wa pili na kikao cha sita cha Baraza la Wafanyakazi wa Wakala huo mkoani Morogoro ambacho kilijadili na kupitia mpango kazi wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2025/2026.
Mhandisi Saidy amesema wakala huo kwa sasa unatekeleza mradi mkubwa wa kupeleka umeme kwenye vitongoji 7,500 na kazi hiyo inaendela kufanyika na itakamilishwa ndani kipindi cha miaka miwili.
Amesema licha ya kazi ikiendelea kwenye vitongoji hivyo kuendelea, Wakala huo unatarajia kuanziasha mradi mpya mwingine mkubwa wa kupeleka umeme kwenye vitongoji 9,000 nchini.
“Kwa sasa kazi inaendelea kupeleka umeme kwenye vitongoji 7,500 ndani ya miaka miwili na hivi sasa tuna mradi mpya mwingine wa kupekela umeme kwenye vitongoji 9,000 na hii itaifanya REA ndani ya miaka mitatu tumefikisha umeme kwenye vitongoji 16,500 “ amesema Mhandisi Saidy.
“ Nasema watu wasiichukulie”powa” REA , sisi tunafanya kazi na hili si jambo ndogo ninawapongeza wafanyakazi wa Wakala kwa kazi hii “ amesisitiza .
Kwa mujibu wa Tovuti ya Ofisi ya Rais , Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) hadi sasa nchi yetu ina Mikoa 26, Wilaya 139, Halmashauri 184, Tarafa 570, Kata 3,956, Vijiji 12,319, Vitongoji 64,384 pamoja na Mitaa 4,263.

Mkurugenzi mkuu wa Wakala huo amesema ,REA ina matarajio makubwa ya kufanikisha miradi hiyo kutokana na mifumo uliyowekwa ya kuwasimamia wakandarasi namna ya kuwajibika baada ya kuingia nao mikataba ya utekelezaji wa miradi hiyo ya kimkakati.
Katika hatua nyingine Mhandisi Saidy amesema ili kuwawezesha wananchi wa vijijini kutumia nishati safi ya kupikia Wakala huo umeanzisha mradi wa ugawaji majiko banifu ikiwa ni njia moja wapo kupunguza upotevu wa misituna kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Mhandisi Saidy amesema mradi huo umefanikiwa kuwafikia wananchi 5,000 wa maeneo mbalimbali ya vijijini na wengine 300,000 wakitarajia kufikiwa na majiko hayo hivi karibuni baada ya Wakala kusaini mikataba ya usambazaji majiko hayo.
Amesema mradi huo unalenga kuwasiadia wananchi wa maeneo ya vijijini ambao hawana uwezo wa kumudu gharama za kununua nishati ya gesi ukilenga pia kupungua athari za uharibifu wa mazingira.
“Changamoto ya gesi ni kwamba ikiisha itabidi utoe fedha kupata nyingine, lakini tunafahamu hali za wananchi wetu kulipa Sh 22,000 wakati mwingine ni mtihani “ amesema .
“ Mtumiaji wa gesi hatashawishika kununua nyingine wakati akitoka ndani ya nyumba yake anakutana na msitu hapo ndio mwanzo wa kukata miti ili apate kuni za kupikia”, amesema Mhandisi Saidy.
Mhandisi Saidy amesema majiko hayo banifu yametengenezwa kitaalamu na kupata kibali kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) yatatumia kiwango kidogo cha mkaa unaozalishwa na malighafi nyingine mbadala kama pumba .
“ Majiko haya banifu ni tofauti na majiko ya mafiga matatu ambayo hutumia kuni na hutoa moshi mwingi na kusababisha athari za kiafya kwa watumiaji” alisema
Kwa upande wake Mwakilishi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya (TUGHE) Taifa, Dk Elias Mtungilwa,amesema ni chama hicho kinawajibu wa kusimamia na kulinda haki na maslahi ya wafanyakazi.



