IMF yaipa tano TRA

DAR ES SALAAM: Ujumbe wa Shirika la Fedha Duniani (IMF) ukiongozwa na Thabo Letjama umekutana na kufanya mazungumzo na Menejimenti ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ikiongozwa na Kamishna Mkuu, Yusuph Juma Mwenda jijini Dar es Salaam kuhusu masuala mbalimbali ya kikodi.

Katika mazungumzo hayo kiongozi wa ujumbe wa IMF, Thabo Letjama, amesema IMF inaridhishwa na utendaji kazi wa TRA na kuwapongeza kwa kuendelea kufanya usimamizi mzuri wa kodi na kuwezesha biashara na uwekezaji nchini.
Aidha, ameipongeza TRA kwa kuwa karibu na Walipakodi na kuahidi kuendeleza uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo baina ya TRA na IMF kwenye kuwezesha biashara, uwekezaji na Utawala wa Kodi.

Kwa upande wake Kamishna Mkuu Mwenda amesema TRA imeimarisha na kuboresha zaidi mahusiano mazuri na walipakodi kote nchini hali ambayo imeongeza kwa kiasi kikubwa uhiari katika kulipa Kodi na kuongeza makusanyo ya Kodi.
Amesema TRA pia imekuwa ikifanya juhudi za kuongeza wigo wa kodi kwa kusajili walipakodi wapya huku ikiwezesha biashara na shughuli nyingine za uchumi sambamba na kuendelea kuimarisha mifumo ya kodi ya kidigitali kupitia IDRAS kwa Kodi za ndani na TANCIS kwa upande wa Forodha.

Mwenda amesema TRA itaendelea kushirikiana na IMF na kuboresha usimamizi katika utawala wa kodi kwa kulioa kwa wakati marejesho ya Kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa walipakodi wenye vigezo.



