Kituo cha mafuta EACOP kukamilika Septemba

KAGERA: Ujenzi wa Kituo cha Kusukuma Mafuta Ghafi Namba Tatu (PS3) cha Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), kilichopo katika Kijiji cha Kikagate, Kata ya Mubunda, Wilaya ya Muleba mkoani Kagera, umefikia asilimia 88 na unatarajiwa kukamilika Septemba mwaka huu.
Wabia na wadau wa mradi wamefanya ziara na kutembelea kituo hicho kwa ajili ya kukagua hatua iliyofikiwa katika ujenzi ambapo Kituo cha PS3 ni kituo cha kwanza cha kusukuma mafuta ghafi kwa upande wa Tanzania na kufikia kiwango hicho cha utekelezaji.

Mkurugenzi wa Mipango na Uwekezaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Derick Moshi, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa TPDC, amewapongeza wakandarasi kwa hatua kubwa iliyofikiwa katika ujenzi wa kituo hicho.

Amesema TPDC, inamiliki asilimia 15 ya hisa katika mradi huo, imepata uzoefu mkubwa kupitia utekelezaji wa EACOP, hususani katika ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati.

Mradi wa EACOP unamilikiwa na TotalEnergies yenye asilimia 62, TPDC asilimia 15, Uganda National Oil Company (UNOC) asilimia 15 na CNOOC Limited ya China yenye asilimia 8.

Kwa upande wake, Meneja wa Kituo cha Kusukuma Mafuta Ghafi Namba Tatu, Dmitry Malyshev, amesema ujenzi wa kituo hicho ulianza Aprili 2024 na ulitarajiwa kukamilika Julai 2026, lakini changamoto za upatikanaji na ucheleweshaji wa baadhi ya malighafi zilisababisha kazi kuchelewa.



