Muswada wa Marekebisho Sheria mbalimbali wapitishwa

DODOMA; Bunge limepitisha Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2026 (The Written Laws (Miscellaneous Amendments) Bill, 2026).
Muswada huo uliwasliishwa bungeni leo Septemba 1, 2026 asubuhi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari, aliyesema mapendekezo ya marekebisho ya sheria 21 ni miongoni mwa hatua muhimu za Serikali katika kuweka mazingira wezeshi ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
“Dira hiyo inalenga, pamoja na mambo mengine, kujenga uchumi imara, jumuishi na shindani unaoenda sambamba na kuwa na taasisi zenye ufanisi, mazingira bora ya biashara na uwekezaji, uwazi na uwajibikaji.
“Ili kufikia azma hiyo, ni muhimu mfumo wa sheria uendelee kuhuishwa ili kuendana na mabadiliko ya kiuchumi, kijamii, kiteknolojia na kimataifa, kuondoa vikwazo vya utekelezaji na kuimarisha mifumo ya usimamizi,” amesema.
Hata hivyo, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, amesema baada ya mashauriano kati ya Serikali na Kamati ya Utawala, Katiba na Sheria, amependekeza kuondolewa kwa baadhi ya marekebisho sheria nne, hivyo kubaki sheria 17.
Ametaja marekebisho hayo ni yaliyokuwa yakihusu Sheria ya Benki Kuu ya Tanzania na Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani, kutokana na masuala hayo kushughulikiwa kupitia Muswada wa Fedha wa mwaka 2026.
Mengine ni marekebisho yaliyopendekezwa katika Sheria ya Usimamizi wa Mahakama na Sheria ya Baraza la Vijana la Taifa yamependekezwa kuondolewa ili kutoa nafasi kwa serikali kuyafanyia kazi zaidi.



