BoT yatoa wito kutunza fedha

MOROGORO: Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imewataka wananchi kuwa na uchungu na fedha zao kwa kuzitunza na kuhakikisha zinabaki katika hali nzuri ili ziendelee kutumika kwa muda mrefu.
Wito huo umetolewa leo Septemba 17, 2026 na Meneja wa Huduma za Kibenki na Sarafu Tawi la Dodoma, Nolasco Maluli katika semina na watu wenye mahitaji maalumu mkoani Morogoro.

“Tunaendelea kutoa elimu kwa Watanzania na jamii kwa ujumla tuwe na uchungu na fedha zetu. Tuzitunze, hii ni tunu ya Taifa, hairuhusiwi kuziharibu kwa namna yoyote,” amesema Maluli wakati akitoa wasilisho kwa kundi hilo.

Kauli hiyo inaungwa mkono na Kifungu cha 332A cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 toleo lililofanyiwa marekebisho Mwaka 2023 ambacho kinamkataza mtu ambaye, bila mamlaka na kwa makusudi, anaharibu, anachanachana, anakata au kwa namna nyingine anaharibu noti ya fedha.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya SEED TRUST, Margaret Agnes Mkanga alisisitiza umuhimu wa elimu ya masuala ya fedha kwa kundi hilo katika kufanikisha kutimiza dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050.

Naye, Mratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, Simfonsa Mollel ameishukuru BoT kwa kuifikisha elimu hiyo kwa makundi maalumu inayosaidia kujenga uchumi jumuishi.



