Jaji Mku: Mchakato kuwapata majaji ni huru

 

JAJI Mkuu wa Tanzania, Prof. Ibrahim Juma, amesema mchakato wa kuwapata majaji nchini ni huru na wazi kwa kuwa unazingatia taratibu na misingi iliyowekwa na Tume ya Mahakama.

Akizungumza wakati wa uapisho wa majaji 21 katika Ikulu ya Chamwino, Dodoma leo,  Jaji Mkuu amesema kumekuwa na upotoshaji mkubwa katika habari za mitandaoni kuhusu mchakato wa kupata Majaji nchini.

“Mitandao ya kijamii haitoi taarifa sahihi, Katiba yetu imeweka kiwango cha chini cha kuwa na Majaji 30, ili tuwe na Mahakama Kuu. Hata hivyo idadi ya ziada inatokana na mahitaji ya Mahakama,” amesema Profesa Juma na kuongeza kuwa:

“Anayejua mahitaji ya majaji ni Jaji Kiongozi ambaye huleta hoja ndani ya Tume ya Mahakama.”

Majina ya majaji wanaoteuliwa hupendekezwa kutoka sekta ya sharia, ikihusisha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na Taasisi za Umma.

Amesema Tume huwaandikia wadau kupendekeza majina ambayo baadaye huchambuliwa kwa kuzingatia vigezo, kisha kupelekwa katika ofisi ya Rais kwa uteuzi.

Katika uteuzi wa hivi karibuni, Tume ilipokea majina 232 ambapo majina 57 yalikidhi vigezo na kuunganishwa kwenye kanzidata ya mahakama kwa ajili ya uteuzi.

Mchanganuo wa majina hayo unahusisha maofisa 87 kutoka ndani ya mahakama, Mawakili wa serikali 30, vyuo vya elimu ya juu 22, Mawakili wa kujitegemea 53, wizara, idara na taasisi za umma 40.

Habari Zifananazo

Back to top button