1,499 wakutwa na matatizo ya macho mikoa miwili

DAR ES SALAAM; JUMLA ya watu 1,499 kati ya 3,800 waliofanyiwa uchunguzi wa magonjwa mbalimbali katika huduma za matibabu bure yaliyoandaliwa na Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila kwa kushirikiana na Vodacom Tanzania wamepatikana kuwa na matatizo ya macho.
Huduma hizo zilifanyika katika mikoa ya Tanga na Kilimanjaro kuanzia Julai 21 hadi 27, 2025 ambapo wananchi takribani 3,800 walinufaika na huduma za uchunguzi na matibabu ya kibingwa na ubingwa bobezi bure.

Daktari bingwa wa macho, Joachim Kilemile amesema kati ya wagonjwa hao walibainika kuwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ukavu wa macho, mzio, uoni hafifu, kushindwa kusoma maandishi madogo ya karibu, mtoto wa jicho na shinikizo la macho.
“Sababu kubwa inayochangia watu kupata changamoto za macho katika maeneo hayo, kwa watu tuliowafanyia uchunguzi inaonekana ni uzee, kisukari pamoja na shinikizo la juu la damu,”ameeleza.

Aidha katika kambi hiyo wanachi waliofanyiwa uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya ndani ni 1,207, Afya ya kina mama na uzazi ni 867.
Kwa upande wa masikio, pua na koo ni 803, tathmini ya watu wenye ulemavu ni 813, huduma ya afya ya watoto ni 700, afya ya kinywa na meno ni 671, saratani 756, ngozi 621 na afya ya akili ni watu 553.



