Washiriki kozi ndefu NDC-TZ wafundwa

DAR ES SALAAM: Washiriki wa Kozi Ndefu katika Chuo cha Taifa cha Ulinzi Tanzania (NDC-TZ) leo wamepatiwa mhadhara maalum ulioangazia mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya uchumi wa Taifa, kwa lengo la kuwaimarisha uelewa wao kuhusu masuala ya uchumi na biashara.

Mhadhara huo uliwasilishwa na Rais wa Chemba ya Taifa ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TNCC), Vicent Minja, akiwa ameambatana na Ofisa Mtendaji Mkuu wa chemba hiyo, Oscar Kissanga.

Mhadhara huo ulihudhuriwa na washiriki 72 wa Kozi Ndefu kutoka mataifa 17, yakiwemo mataifa ya Afrika na nje ya Afrika.

Mada kuu iliangazia nafasi ya kimkakati ya sekta binafsi katika kukuza uchumi pamoja na umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa karibu kati ya sekta binafsi na Serikali kama msingi wa maendeleo endelevu ya Taifa.

Akizungumza wakati wa mhadhara huo, Minja amesema kuwa ukuaji wa uchumi endelevu hauwezi kufikiwa bila uwepo wa sekta binafsi imara inayoshirikiana kwa karibu na Serikali katika utekelezaji wa sera na mipango ya maendeleo.

Amesisitiza pia umuhimu wa kuongeza thamani ya rasilimali za ndani barani Afrika ili kuongeza ushindani wa bidhaa za Kiafrika, kukuza viwanda, kuimarisha matumizi ya teknolojia na kuendeleza ujuzi wa wazawa.

Kwa upande wake, Mkufunzi Mwandamizi Elekezi wa Jeshi la Wanamaji katika chuo hicho, Brigedia Jenerali Baga Traseas Rutambuka, ameipongeza TNCC kwa kutoa mhadhara wenye manufaa makubwa.

Ameeleza kuwa uelewa mpana wa masuala ya uchumi na biashara ni muhimu kwa washiriki wa NDC-TZ kama sehemu ya maandalizi yao ya uongozi wa kijeshi na kiraia.

Katika hatua nyingine, TNCC imeeleza kuwa itaendelea kushirikiana na taasisi za kitaifa na kimataifa katika kuendeleza biashara, uwekezaji na ukuaji wa sekta binafsi, kwa lengo la kukuza maendeleo jumuishi na endelevu ya Taifa na Bara la Afrika kwa ujumla.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button