Shigela mgeni rasmi Siku ya Punda Duniani

MKUU wa Mkoa wa Geita, Martin Shigela anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Punda Duniani yatakayofanyika kitaifa Mei 8, 2026 katika Kijiji cha Mgusu, Manispaa ya Geita.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, maandalizi ya tukio hilo yamekamilika, huku shughuli za awali zikitarajiwa kuanza Mei 6 hadi 7 kwa kutoa huduma za matibabu kwa punda pamoja na elimu kwa wafugaji na jamii.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa kipindi hicho, kliniki maalumu zitahudumia takribani punda 700 katika maeneo ya Mgusu, Magenge na mji wa Geita. Sambamba na hilo, elimu kuhusu utunzaji bora, lishe na matumizi sahihi ya vifaa vya punda itatolewa ili kuboresha ustawi wa wanyama hao.

“Zaidi ya wanafunzi 3,800 pamoja na wanajamii watanufaika na programu za elimu zitakazowasilishwa kupitia maonesho ya vitendo, sanaa na kampeni za uhamasishaji, lengo likiwa ni kujenga kizazi chenye uelewa wa kulinda rasilimali hiyo muhimu,”ilieleze taarifa hiyo.

Maadhimisho hayo yatakuwa jukwaa muhimu la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa ustawi wa punda, yakiongozwa na kaulimbiu isemayo, “Kulinda Punda wa Afrika ni Wajibu Wetu Sote.” Kaulimbiu hiyo inalenga kuibua uelewa mpana juu ya changamoto zinazowakabili punda na haja ya kuchukua hatua za pamoja kuwalinda.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button