Tanzania yasihi dunia kukabili changamoto za mazingira
SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetoa wito kwa Jumuiya ya Kimataifa kuchukua hatua za haraka, shirikishi na zenye matokeo katika kukabiliana na changamoto za mazingira zinazoendelea kuikabili dunia.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Watu wenye Ulemavu) William Lukuvi ametoa wito huo katika hotuba aliyoitoa kwa niaba ya, Rais Samia Suluhu Hassan katika kikao cha ngazi ya juu cha Mkutano wa Saba wa Baraza la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEA-7), kinachoendelea jijini Nairobi, Kenya.
Katika hotiba hiyo, Lukuvi ameeleza kuwa kaulimbiu ya mkutano huo inaakisi wazi changamoto kubwa za mazingira zinazoukumba ulimwengu kwa sasa zikiwemo kupungua kwa bioanuwai, ongezeko la uchafuzi wa mazingira, na shinikizo katika rasilimali asilia ni hali halisi inayoathiri maisha ya mamilioni ya watu duniani.
“Dalili za tahadhari ziko wazi kabisa. Hatuwezi tena kuziangalia kwa mbali. Tunahitaji uongozi thabiti, unaotegemea ushahidi wa kisayansi na unaojengwa juu ya mshikamano wa kimataifa,” amesema.
Akiainisha mwelekeo wa kimkakati wa Tanzania katika mazingira, Lukuvi amesema kuwa unaongozwa na Dira ya Taifa 2050, Sera ya Taifa ya Mazingira, pamoja na Mikakati na Mipango mingine.
Aidha, katika kufanikikisha mwelekeo huo, alibainisha kuwa Tanzania inaendelea kuongeza matumizi ya nishati safi na salama, ikijumuisha nishati safi ya kupikia, kuimarisha uhifadhi wa misitu, ardhi oevu na ukanda wa pwani; sanjari na kuendeleza kilimo kinachohimili mabadiliko ya tabianchi.
Lukuvi alisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kujenga uthabiti wa sekta ya mazingira, akisema kuwa hakuna taifa linaloweza kujenga ustahimilivu peke yake bali unahitajika ushirikiano, usawa katika upatikanaji wa teknolojia, pamoja na vyanzo vya fedha vya uhakika na vinavyotabirika.
Halikadhalika, alisema kwa nchi nyingi zinazoendelea, ikiwemo Tanzania, changamoto za mazingira mara nyingi huzidi uwezo wa kukabiliana nazo, hivyo, aliziomba nchi washirika kutimiza ahadi zao katika kuzisaidia nchi hizo.



