Aliyedaiwa milioni 21/- malazi, chakula Serena aachiwa huru

DAR ES SALAAM; MAHAKAMA ya Mwanzo ya Kariakoo, Dar es Salaam imemwachia huru mkazi wa Goba Kulangwa, Denis Mfumbulwa (44) katika kesi ya kudaiwa kutolipa Sh 21,491,866.97 za huduma ya malazi na chakula katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam.
Hakimu Gladness Njau alitoa hukumu hiyo jana wakati kesi hiyo ilipokwenda kwa ajili ya kusikilizwa. Mshitakiwa baada ya kufika mahakamani hapo alipewa nafasi ya kujitetea kutokana na mashtaka yanayomkabili.
“Nakiri kutenda kosa hilo na niko tayari kumlipa mlalamikaji hivyo naomba nafasi nizungumze naye,”
alidai.
Baada ya kusikiliza utetezi huo hakimu alitoa nafasi kwa mlalamikaji na mshtakiwa kuzungumza ili kufikia mwafaka pia yeye (hakimu) apate nafasi ya kupitia kesi hiyo kiundani na baada ya muda mfupi warejee mahakamani hapo.
Muda ulipofika wa kurejea mahakamani Hakimu Njau alidai amelipitia jalada la kesi hiyo na amejiridhisha
kuwa kesi hiyo si ya jinai bali ni madai. Akisoma hukumu hiyo Njau alisema: “Kesi hii haina ushahidi wa kijinai hivyo mahakama inamuachia huru mshtakiwa na hatuwezi kuendelea kusikiliza shauri hili, sababu ya shauri hili kuwa na sifa zote za madai, hivyo mlalamikaji kama utaona inafaa na upate haki yako fungua kesi nyingine ya madai”.
Akizungumza nje ya mahakama, mlalamikaji Desdery Dotto alidai kuwa yupo tayari kuendelea na kesi hiyo. “Nitaenda kufungua shauri la madai ili nipate haki yangu, hapa nasubiri nakala za hukumu ili niendelee,” alidai Dotto.
Mei 13, mwaka huu mshtakiwa Denis alifikishwa mahakamani hapo akikabiliwa na mashtaka ya kujipatia huduma ya malazi na chakula yenye thamani ya Sh milioni 21.4 katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam na kutoweka bila kulipa.
Mshtakiwa alisomewa mashtaka yake na Karani Aurelia Bahati. Karani Bahati alidai kuwa Machi 6, 2022 hadi Machi 28, 2024 kwa nyakati tofauti katika Hoteli ya Serena Mtaa wa Ohio Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam, mshtakiwa alijipatia huduma ya malazi na chakula yenye thamani ya Sh 21,491,866.97 bila kulipa mali ya mlalamikaji Desdery Dotto na hatimaye kutoweka huku akijua kuwa kitendo hicho ni kinyume na sheria.
Mshtakiwa baada ya kusomewa mashtaka yanayomkabili alikana kutenda kosa hilo.