Bandari ya Dar kuongeza idadi ya gati

DODOMA; SERIKALI imesema kutokana na ongezeko la meli na shehena kwa ujumla, Bandari ya Dar es Salaam inaendelea na mipango kuongeza idadi ya gati, vifaa na mifumo stahiki ili kukabiliana na hali hiyo.
Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, ametoa kauli hiyo alipokuwa akijibu swali la mbunge wa Bumbwini, Mwinyi Jamal Ramadhan aliyehoji kwa nini Bandari ya Dar es Salaam inashindwa kupokea meli nyingi kwa wakati mmoja.
“Upokeaji wa meli katika gati za bandari zote duniani hutegemea mambo kadhaa yakiwemo; urefu wa gati kwa meli husika, ukubwa wa yadi ya kuhudumia shehena, kina cha lango la kuingilia meli, vifaa vya kuhudumia shehena, mifumo ya kuhudumia meli na shehena iliyo fungamanishi, aina na ubora wa barabara na reli zinazoingia na kutoka bandarini, kasi ya ongezeko la shehena na mahitaji ya meli, pamoja na mambo mengine.
“Kwa sasa Bandari ya Dar es Salaam inazo gati 13 zenye uwezo kuhudumia meli za aina ya “Post Panamax” ambazo ni kubwa katika ukanda unaohudumiwa na Bandari za Afrika Mashariki, Kati na Kusini.
“Hata hivyo idadi hii ya gati bado ni ndogo ukilinganisha na kasi ya ongezeko la meli na shehena.
“Aidha, kutokana na ongezeko la meli na shehena kwa ujumla, Bandari ya Dar es Salaam inaendelea na mipango kuongeza idadi ya gati, vifaa na mifumo stahiki ili kukabiliana na hali hiyo.
“Kwa kuanzia ujenzi wa gati la mita 500 katika Bandari ya Dar es Salaam umeanza sambamba na maandalizi ya ujenzi wa gati nyingine nne (gati namba 12-15) ambapo Serikali kupitia Wizara ya Fedha na TPA wameanza mazungumzo ya awali na Benki ya Dunia kwa ajili ya kupata mkopo nafuu kugharamia ujenzi wa gati hizo,” amesema Naibu Waziri.



